Thursday, January 11, 2018

JIONESHE KUWA MWANAMUME


 JIONESHE KUWA MWANAMUME (1 Wafalme 2:1)

Bwana Yesu Kristo apewe sifa. Ninamshukuru Mungu kwa neema Yake kuu amenipatia kibali cha kulihudumia kanisa Lake hata sasa. Leo ninao ujumbe wenye baraka kwako uliobeba kichwa kinachoitwa: JIONESHE KUWA MWANAMUME. Huu ni mwanzoni mwa mwaka 2018, watu wengi wanatazamia baraka nyingi ziambatane nao; hivyo basi, Roho wa Mungu amenipa ujumbe huu kwa ajili yako: “JIONESHE KUWA MWANAMUME”.
Hebu tufungue Biblia zetu tusome 1 Wafalme 2:1-2, Biblia Takatifu inasema:

Basi siku ya kufa kwake Daudi ikakaribia, akamwusia Sulemani mwanawe, akasema, Mimi naenda njia ya ulimwengu wote (yaani, naenda kufa); basi uwe hodari, ujioneshe kuwa mwanamume…” ~ 1 Wafalme 2:1-2

Mfalme Daudi anamwambia Sulemani mwanawe: “…ujioneshe kuwa mwanamume…” (“…show thyself a man…” - KJV)

Je, nini basi maana ya “…kuwa mwanamume…”? Mwanamue ni mtu asiye ogopa, mtu jasiri mwenye kufanya mambo magumu na shujaa. Kuwa mwanamume sio kijinsia bali ni kuwa jasiri na hodari. Mfalme Daudi alitambua dhahili shujaa ndiye anayetawala wala si mtu mlegevu; hapo alimtaka Sulemani mwanawe awe mtu hodari na jasiri ili aweze kuhimili misukosuko ya utawala unaomkabili. Mfalme Daudi sio tu alimtaka Sulemani mwanawe awe hodari, bali pia AJIONESHE YEYE NI HODARI; yaani watu wamwone na wamtambue yeye ni hodari. Hivyo ndivyo Mungu anavyotaka sisi tuwe hadi ulimwengu utambue uwepo wetu (Luka 10:19).

Watu wengi huwa wanatamani sana kuinuliwa, lakini je umejiandaa kuzikabili changamoto zinazoambatana na baraka hizo? Mara zote unapobarikiwa na kuinuliwa kwa viwango vya juu kunaambatana na kundi la maadui linalokupinga kimwili na kiroho; mf. kuna majambazi, pepo wachafu, wachawi, wasengenyaji na wengine watakuchukia tu kwa sababu wewe umeinuliwa juu kuliko wao. Ndio maana neno la kwanza tumeona Sulemani ameambiwa “…uwe hodari…” (1 Fal 2:2; 1 Nya 28:10, 20) Mtu hodani ni yule mwenye uwezo wa kufanya jambo lililowashinda wengine, mtu mahiri na stadi; anayewaongoza watu kwenda pale wanapopaswa kwenda wala si pale wanapotaka kwenda.

Ukitaka kuvifikia viwango vya juu vya Baraka ni lazima uchague kufanya mambo magumu kwa wengine, usichague mambo mepesi mepesi; bali yafanye mambo magumu kwa umahiri na ustadi mkubwa. Uwe hodari katika kila ufanyalo; iwe katika biashara yako, masomo yako, familia yako, ndoa yako, kazi zako na katika kila utendalo.

Sasa hivi tumeshaingia katika mwaka mpya ambao wengi wanatazamia kuinuliwa zaidi ya mwaka uliopita; Lakini tambua kuwa mwaka mpya ni badiliko la kalenda tu, bali kutamalaki hakupo kwa watu walegevu wala wavivu, ila ni kwa watu walio hodari. Lazima ujioneshe kuwa mwanamume.
Biblia inasema:

Atendaye mambo kwa mkono mlegevu huwa maskini; Bali mkono wake aliye na bidii hutajirisha.– Mithali 10:4

Utofauti kati ya fukara na tajiri upo katika namna yake ya kufikiri na jinsi anavyotenda mambo; ni hivyo tu. Utajiri / kufanikiwa ni uchaguzi wako, hata ufukara / kushindwa pia ni uchaguzi wako pia. Huwezi kukwea ngazi ya kamba iliyoning’inia huku ukiwa umeweka mikono mfukoni mwa suluali yako! Ni lazima ushikilie vizuri ndipo utaweza kuikwea.

Hata mafanikio ya mtu hayaji kizembe, ni lazima uchague kufanya mambo magumu, makubwa yanayowashinda wavivu. Uwe na ndoto kubwa, heshimu malengo yako, uwe jasiri, thubutu kutenda bila woga, fanya kile chenye faida, tunza wakati, epuka marafiki wabaya, uwe na nidhamu ya pesa, weka akiba katika vitu vinavyoongezeka thamani na umtangulize Mungu katika kila ufanyalo. Wakati sahihi wa kufanikiwa ni sasa; anza na hicho ulichonacho: kama ni wazo basi washirikishe watu sahihi, na kama ni mtaji kidogo anza nao uo huo huku ukiwa na mipango ya kufika juu zaidi.

Vile vile tambua kwamba, hauwezi kufanikiwa kwa akili zako mwenyewe tu; ndio maana mfalme Daudi anaendelea kumwambia Sulemani mwanawe, kwamba:

“…uyashike mausia ya BWANA, Mungu wako, uende katika njia Zake, uzishike sheria Zake, na amri Zake, na hukumu Zake, na shuhuda Zake …upate kufanikiwa katika kila ufanyalo, na kila utazamako.” 1 Wafalme 2:3-4

Mweke Mungu mbele ya kila jambo; Ndio maana sisi tunaambiwa: “Na kila mfanyalo, kwa neno au kwa tendo, fanyeni yote katika jina la Bwana Yesu, mkimshukuru Mungu Baba kwa Yeye. “ – (Wakolosai 3:17). Ukimtumainia Mungu katika yote, hapo ndipo kila utazamako (unachokihitaji) kinakuwa chako. Katika kuomba kwako usiombe kwa tamaa zako, bali kwa ajili ya utukufu wa Mungu (Yakobo 4:3). Lazima Mungu awe na sehemu katika mipango yako, na zingatia kumtolea Mungu sadaka ya shukurani katika mapato yako; si kwa kulazimishwa, bali kwa moyo mkunjufu wa shukurani sawa sawa na jinsi Mungu alivyokubariki. Endapo kama umemuwekea Mungu nadhiri, hakikisha unakuwa mwaminifu katika kuitimiza kwa uhaminifu wote (Hesabu 30:2; Kumb 23:21).
Uwe hodari katika kila lililo jema wala si katika uovu (Zaburi 64:5), ndio maana Biblia inasema:

“…Heri mtu yule amchaye BWANA, Apendezwaye sana na maagizo Yake. Wazao wake watakuwa hodari duniani; Kizazi cha wenye adili kitabarikiwa.” – Zaburi 112:1-2

Hapo zingatia neno hili: “Kizazi cha wenye adili kitabarikiwa.” Hicho ni kizazi kinachomtii Mungu ndicho kinachobarikiwa. Baraka za mcha Mungu hodari zitaambatana naye pamoja na kizazi chake. Sisi Wakristo, tayari Mungu ametubariki wala hakuna laana yoyote ile inayotuandama (1 Petro 2:9). Japokuwa tayari Mungu amekubariki, kama jinsi tunavyosoma katika Kumb 28:2-6

…baraka hizi zote zitakujilia na kukupata usikiapo sauti ya BWANA, Mungu wako. Utabarikiwa mjini, utabarikiwa na mashambani. Utabarikiwa uzao wa tumbo lako, na uzao wa nchi yako, na uzao wa wanyama wako wa mifugo, maongeo ya ng'ombe wako, na wadogo wa kondoo zako. Litabarikiwa kapu lako, na chombo chako cha kukandia unga. Utabarikiwa uingiapo, utabarikiwa na utokapo. – Kumb 28:2-6

Lakini baraka hizi utazipata pale USIPOKATA TAMAA. Hakuna mafanikio mepesi, ni lazima kuwa hodari kweli kweli; lazima ujioneshe kuwa mwanamume kweli kweli. Hebu tusome habari hii itakusaidia kukufungua ufahamu wako; katika Mwanzo 26:17-22 Biblia inasema:

Basi Isaka akatoka huko akapiga kambi katika Bonde la Gerari, akakaa huko. Isaka akarudi akavichimbua vile visima vya maji walivyovichimba siku za Abrahamu babaye, maana wale Wafilisti walikuwa wamevifukia baada ya kufa kwake Abrahamu. Naye akaviita majina kufuata majina alivyoviita babaye. Pia watumishi wa Isaka wakachimba katika lile bonde, nao wakapata kisima cha maji yanayobubujika.
Bali wachungaji wa Gerari wakagombana na wachungaji wa Isaka, wakisema, “Maji haya ni yetu.” Ndipo akakiita jina la kile kisima Eseki, kwa sababu waligombana naye. Nao wakachimba kisima kingine, wakagombania na hicho tena. Basi akakiita jina lake Sitna. Akaondoka huko na akachimba kisima kingine, wala hicho hawakukigombania. Basi akakiita jina lake Rehobothi, kwa maana alisema, “Kwa kuwa sasa BWANA ametufanyia nafasi, nasi tutazidi katika nchi.” – Mwanzo 26:17-22

Hapo tumejifunza Isaka hakupoteza muda kung’ang’ania kushindana na adui zake, bali yeye alitazama fursa kwingine na kuitumia. Siku zote ukitaka kufika viwango vya juu vya baraka, usipoteze muda kushindana na mtu mpumbavu, bali tazama fursa zilizopo mbele yako alafu piga hatua kuzifuata. Usifanye jambo lisilo na faida kwako, usiupoteze bure wakati wako. Usiishie kulaumu tu, bali tazama fursa zilipo na ujichanganye huko. Baraka za Mungu zinaambata na mtu yule aliyechukua hatua kuzifuata; wala sio kwa kusali tu, wala kwa kufunga na kuomba tu: bali kwa matendo pia. Huwezi kuzifikia baraka zako kwa kuishia kusema “amina” kanisani wala kwa kupewa mafuta ya upako; bali unapaswa utambue tayari Mungu amekwisha kubariki ila kilichobaki ni wewe kuzifuata hizo baraka zako. Hapo ni sawa na mzazi aliyekuwekea chakula ndani, ila wewe umebakiza jukumu lako la kuinuka na kukila pindi unapokihitaji. Tazama wapi fursa zilipo, nawe nenda huko kazifuate ndipo utaifikia baraka yako.

Jambo la mwisho la kuzingatia ninalopenda kukwambia; Tenda mambo kwa busara bila kumdharau mtu awaye yote. Biblia Takatifu inatuambia kwamba:

 “Tazama, Mungu ni hodari, wala hamdharau mtu ye yote; Ana uweza katika nguvu za fahamu.” – Ayubu 36:5

Mungu Mwenyewe ni hodari (yaani, anatenda mambo yanayowashinda wengine) lakini hamdharau mtu ye yote. Hizi mali na utajiri tunaoupata vyote vinatoka Kwake, ni kwa neema Zake tu; hatukuja na kitu duniani na wala hatutaondoka na kitu duniani; hivyo basi tuwahehimu na kuwapenda watu wote, na hata kuwaombea watu walio adui zetu (Luka 6:35; Warumi 12:20).
Tukisoma katika Mithali 17:2 tunaona Biblia inasema:

“Mtumwa atendaye kwa busara atamtawala mwana atendaye mambo ya aibu; Tena atapata sehemu ya urithi kati ya ndugu.” – Mithali 17:2

Zingatia point hii: hapo (Mithali 17:2) imetumia neno "Mtumwa...", kwa kumaanisha "mtu mwovu" (yule asiyemtii wala kumwabudu Mungu wa kweli) akitenda mambo kwa busara ndipo atamtawala "...mwana..."  atendaye mambo ya aibu (mtu wa Mungu aliyekengeuka au afanyaye mambo kivivu).  Kwa hiyo; hapo neno "mtumwa" linamwakilisha "mtu mwovu", na neno "mwana" linamwakilisha "mtu wa Mungu". Hapa ndipo utaweza kuwaona baadhi watu waovu wanafanikiwa na kustawi maishani kuliko wacha Mungu walio wavivu; ndiyo maana hapo Biblia inamalizia kwa kusema kuhusu huyo mtumwa: "..Tena atapata sehemu ya urithi kati ya ndugu.” – (Mithali 17:2) Yaani atamiliki ile sehemu uliyopaswa wewe kuipokea.

Mafanikio au kushindwa vyote vipo katika uchaguzi wako; ikiwa unahitaji kufanikiwa, basi tenda mambo yote kwa busara, hekima na uwe hodari. Hakuna mafanikio yanayokuja kizembe; ni lazima ujioneshe kuwa mwanamume (sio kijinsia, ila katika “attitude” yako – namna yako ya kufikiri na kutenda kama mwana wa mfalme).


Jina langu naitwa Masanja Sabbi (masanjasabbi@gmail.com), nakutakia kheri na baraka tele katika kila utendalo. Malaika wa Mungu akutangulie na kukufanikisha katika jina la Yesu Kristo. Amen.

0 MAONI:

Post a Comment

TUMA KWA RAFIKI :

Twitter FacebookMore

 
Kuhusu Huduma Hii | Masharti Ya Utumiaji Wa Tovuti Hii | Wasiliana Nasi | Tangaza Kupitia Tovuti Hii