MPOKEE YESU

sparkle effect online

sparkle photo effect
Yesu anakupenda.

Je! Unataka kumpa Yesu maisha yako sasa hivi ili akuokoe na kukupatia uzima wa milele? Je! Unajua maana ya kumpokea Yesu maishani mwako?
Kumpokea Yesu maana yake ni KUKIRI kwamba Yesu ni MWOKOZI, na pia hakuna mwingine awezaye kuokoa isipokuwa Yesu pakee. Biblia Takatifu inatuambia kwamba:

Wala hakuna wokovu katika mwingine awaye yote, kwa maana hapana jina jingine chini ya mbingu litupasalo sisi kuokolewa kwalo.” (Matendo 4:12)

Ni Yesu pekee anayetuokoa wala si mtu mwingine ye yote yule. Wapo watu wengine wanaokiri kwamba Yesu ni Mwokozi lakini bado wanasema kuwa wapo wanadamu wengine wanaoweza kuwaokoa badala ya Yesu; huko ni sawa na wanajidanganya wao wenyewe na tena wanapotea japokuwa wanajiita Wakristo. Kuwa mfuasi wa Yesu ni kushika “...YOTE...” na kuwafundisha watu kushika “...YOTE...” ambayo Yesu ametuamuru sisi bila kuongeza neno wala kupunguza neno (Mathayo 28:20). Hatuokolewi kwa jina la Mariamu mama wa Yesu wala kwa jina la mtakatifu ye yote yule; bali hao tunawaheshimu kwa kutambua na kuuthamini mchango wao katika huduma ya Mungu sawa sawa na jinsi ambavyo tunavyowaheshimu watumishi wengine wote wa Mungu, lakini wokovu upo kwa Yesu pekee. Hilo ndilo neno la Mungu lisemavyo, na tena imeandikwa:

...Imetupasa kumtii Mungu kuliko wanadamu.” (Matendo 5:29)

Yesu ni Mwokozi kwa sababu wokovu wetu upo kwa Yesu pekee. Wala HAKUNA mtu ye yote yule mwingine aliyeutoa uhai wake kwa ajili ya msamaha wa dhambi zetu; bali ni Yesu pekee. Unapompokea Yesu unakuwa umeokoka. Najua hapa unaweza ukahoji kuwa: “Je! Nawezaje kuokoka ningali hai bado humu duniani?” Mpendwa; hayo mawazo uliyonayo ni akili za kibanadamu lakini kwa Mungu wokovu upo sasa wala si baadae. Biblia Takatifu inatuambia kwamba:

...Tazama, wakati uliokubalika ndio sasa; tazama, siku ya wokovu ndiyo sasa.” (2 Wakoritho 6:2)

Je! Nini basi maana ya WOKOVU?

Wokovu maana yake: ni kutoka katika mateso, shida, dhiki, na taabu za kila aina; kisha unapatiwa ulinzi ambao utakuweka salama. Unaweza ukashangaa na ukahoji; “Mbona basi Yesu ametuokoa alafu bado tunaishi katika dunia hii yenye tabu na mateso mengi?
Mateso na tabu hizi za duniani ni za muda mfupi tu. Na pia Mungu ameruhusu sisi tuwemo humu duniani ili tufanye kazi ya kuhubiri neno la Mungu kwa watu wale ambao bado hawajalipokea ili nao wapate kuokoka (Yohana 17:15-17). Wakati huu ni wa muda mfupi tu, na baada ya hapa tutapewa maisha ya uzima wa milele yasiyokuwa na shida, tabu, wala mateso ya namna yo yote ile. Biblia Takatifu inatuambia kuwa Mungu:

...atafuta kila chozi katika macho yao, wala mauti haitakuwapo tena; wala maombolezo, wala kilio, wala maumivu hayatakuwapo tena...” (Ufunuo 21:4)

Dhiki hizi za duniani ni matokeo ya vita dhidi yetu na Shetani. Vile vile Yesu hajatutelekeza hapa duniani bali ametuachia ulinzi wa Mungu unaotuwezesha sisi kuishi salama japokuwa tupo katika dunia yenye majaribu. Bwana Yesu ametuambia kwamba:

...mpate kuwa na amani ndani Yangu. Ulimwenguni mnayo dhiki; lakini jipeni moyo, Mimi nimeushinda ulimwengu.” (Yohana 16:33)
Wokovu huu tulionao unamaana ya kwamba:
Þ           Wokovu ni msamaha wa dhambi ambao Yesu ametupatia baada ya kufa msalabani kwa ajili ya ondoleo la dhambi zetu. Msamaha huu wa dhambi tunaupokea bure kwa njia ya imani na neema tu kwa kumkiri Yesu kuwa Yeye ni Bwana na Mwokozi wa maisha yetu. Biblia Takatifu inatuambia kwamba:
Kwa maana mmeokolewa kwa neema, kwa njia ya imani; ambayo hiyo haikutokana na nafsi zenu, ni kipawa cha Mungu; wala si kwa matendo, mtu awaye yote asije akajisifu.” (Waefeso 2:8,9)
Biblia imesema: “...MMEOKOLEWA...” maana yake ni tayari huo wokovu tunao hivi sasa. Laiti kama wokovu tungekuwa bado hatujaupata basi hapo pangeandikwa “...MTAOKOLEWA...” Lakini kwa kuwa tayari wokovu huu tunao ndio maana hapo pameandikwa: “...MMEOKOLEWA...” Wokovu huu ni BURE kwa njia ya IMANI na KUKIRI kuwa Yesu ni Bwana na Mwokozi wa maisha yako (Matendo 16:31).
Þ           Wokovu huu ni ushindi ambao Yesu ametupatia na kutuwezesha kuharibu kila kazi ya Shetani na kumshinda Shetani kutokana na Roho Mtakatifu akaaye ndani yetu. Bwana Yesu ametuambia kwamba:
Tazama, nimewapa amri ya kukanyaga nyoka na nge, na nguvu zote za yule adui, wala hakuna kitu kitakachowadhuru.” (Luka 10:19)
Japokuwa tunapita katika majaribu mbalimbali humu duniani lakini Yesu ametuwezesha kumshinda Shetani. Shetani tayari amekwishashindwa, kilichabaki ni sisi tu kumkemea Shetani naye lazima atatii; kwa maana imeandikwa: “...Mpingeni Shetani, naye atawakimbia.” (Yakobo 4:7). Hivyo wokovu tulionao sasa umetupatia nguvu ya Mungu itupatiayo ushindi juu ya dhambi, Shetani, na pepo wachafu katika maisha yetu ya kila siku.
Þ           Pia, Wokovu huu tulionao ni hakikisho la uzima wa milele tuliopewa tayari na Bwana Yesu baada ya ufufuko wake kwa kuyashinda mauti. Japokuwa miili yetu itakufa lakini tunalo hakikisho la uzima wa milele kwa maana Biblia Takatifu inatuambia kwamba:
...sisi, wenyeji wetu uko mbinguni, kutoka huko tena tunamtazamia Mwokozi, Bwana Yesu Kristo. Atakayeubadili mwili wetu wa unyonge upate kufanana na mwili Wake wa utukufu, kwa uweza ule ambao kwa huo aweza hata kuvitiisha vitu vyote chini Yake.” (Wafilipi 3:20,21)
Kwa hiyo wokovu huu tulionao hivi sasa unatupatia uhakika wa uzima wa milele baada ya uharibifu utakaotokea katika miili hii tuliyonayo hivi sasa. Hivyo ndivyo neno la Mungu linavyosema kuwa “...WAKATI ULIOKUBALIKA NDIO SASA; TAZAMA, SIKU YA WOKOVU NDIYO SASA.” (2 Wakorintho 6:2) Kama wewe unapingana na Biblia Takatifu; basi, wewe mwenyewe utajibu mbele za Mungu kwa nini umepingana na neno Lake.
Dunia tunayoishi imejawa na mafundisho mengi yanayopotosha ambayo yamesababisha mgawanyiko mkubwa wa imani na njia za kumtafuta Mungu wa kweli, na watu wengi wanapotea pasipo hata wao kujitambua kuwa wanapotea. Japokua duniani wapo wapotoshaji wengi, lakini haimaanishi kwamba neno la kweli la Mungu halipo; La! Neno la Mungu la kweli lipo na wala halijabadilika na tena lipo wazi wala halijajificha. Jambo la muhimu linaloweza kukusaidia ni wewe kuwa tayari kulipokea neno hilo la Mungu na pia ukalifanyia kazi kwa kuishi kama jinsi neno la Mungu lisemavyo.
Ni kweli kwamba Shetani yupo vitani dhidi yetu sisi watakatifu na watu wa Mungu tuliopo hapa duniani, lakini sisi hatuwezi kumshinda shetani kwa nguvu na uwezo wetu bali ni kwa nguvu na uweza wa Mungu unaotuwezesha. Hakika tunahitaji msaada wa Yesu maishani mwetu ili tupate uzima wa milele.
Inawezekana kabisa wewe unayesoma ujumbe huu umeshitushwa na maandishi hayo yaliyopo juu ya ukurasa wa somo hili yasemayo “Yesu ni Mungu.” Yawezekana haufahamu hivyo kutokana na mafundisho uliyoyapokea hapo awali; lakini napenda nikuambie neno hili: Kutokufahamu kwako na kukana kwako hakuwezi kuuvua Uungu wa Yesu. Yesu anabaki kuwa Mungu daima na milele yote. Nitakupa ushahidi wa baadhi ya maandiko matakatifu yanayotuthibitishia kuwa Yesu ni Mungu.
Biblia Takatifu inatuambia kwamba:
Twajua ya kuwa sisi tu wa Mungu; na dunia yote pia hukaa katika yule mwovu. Nasi twajua kwamba Mwana wa Mungu amekwisha kuja, naye ametupatia akili kwamba tumjue Yeye aliye wa kweli, nasi tumo ndani yake Yeye aliye wa kweli, yaani, ndani ya Mwana Wake Yesu Kristo. Huyu ndiye Mungu wa kweli, na uzima wa milele.” (1 Yohana 5:19,20)
Hapo tunaona Biblia Takatifu inatuambia: “...Yesu Kristo. Huyu ndiye Mungu wa kweli, na uzima wa milele.” (1 Yohana 5:20). Ukimpokea Yesu unakuwa “...NDANI...” ya Yesu ambaye ndiye Mungu wa kweli, pia ni Mwokozi wetu na uzima wa milele. Pia Biblia Takatifu inatuambia kwamba:
Tukilitazamia tumaini lenye baraka na mafunuo ya utukufu wa Kristo Yesu, Mungu mkuu na Mwokozi wetu, Ambaye alijitoa nafsi Yake kwa ajili yetu, ili atukomboe na maasi yote na kujisafishia watu wawe milki Yake Mwenyewe, wale walio na juhudi katika matendo mema.” (Tito 2:13,14)
Napo hapo pia tumeona Biblia Takatifu inasema: “...Kristo Yesu, Mungu mkuu na Mwokozi wetu...” (Tito 2:13,14). Biblia Takatifu inatuthibitishia kwamba Yesu ni Mungu; tena Biblia Takatifu imesema wazi wazi kabisa bila uficho kuwa Yesu ni Mungu. Yawezekana na hapo pia ukapata maswali mengi, mfano:
Inawezekanaje Yesu awe Mungu wakati alizaliwa na kuishi kama mwanadamu?
Ni kweli jambo hili pia nalo huwashinda watu wengi kulielewa; Wapo watu waonakiri kuwa Yesu ni Bwana lakini wanakana kwa kusema Yesu si Mungu. Ukweli ni kwamba Yesu ni Mungu. Je! Yesu ni Mungu kwa vigezo vipi?
Ni vema kwanza kabisa ukafahamu kwamba jina Mungu ni “cheo” ambacho kinazo sifa za kipekee zifuatazo:
        i:            Mwenye hicho cheo cha "Mungu" Yeye hakuumbwa bali alikuwepo na tena hana mwanzo wala mwisho.
      ii:            Mwenye hicho cheo cha "Mungu" Yeye ndiye ameumba mbingu, nchi, na vitu vyote. Yeye ndiye mwanzo wa uhai wote.
     iii:            Mwenye hicho cheo cha "Mungu" Yeye ndiye mwenye amri na mamlaka ya kusamehe dhambi, pasipo Yeye hakuna ondoleo la dhambi.
    iv:            Mwenye hicho cheo cha “MunguYeye ndiye anayo mamlaka ya kuhukumu ulimwengu.
Hizo ndizo sifa za kipekee kabisa ambazo Mungu anazo. Hebu tujifunze; je! Yesu Kristo anazo sifa hizo za Mungu?
Jibu ni “NDIYO” kwa uthibitisho ufuatao:
A.     Yesu Kristo hajaumbwa bali alikuwepo tangu milele yote.
Ni kweli kabisa kwamba Yesu alikuwepo tangu milele yote kabla ya kuumbwa kitu cho chote kile. Bwana Yesu kwa kauli ya kinywa chake mwenyewe anasema kwamba:
Na sasa, Baba, unitukuze Mimi pamoja Nawe, kwa utukufu ule Mimi niliokuwa nao pamoja Nawe kabla ya ulimwengu kuwako.” (Yohana 17:5)
Neno “UTUKUFU” maana yake ni heshima, uweza, uzuri, umaarufu, nguvu, sifa na mamlaka. Mambo hayo yote Yesu alikuwa nayo kabla hata ulimwengu haujaumbwa. Yesu Kristo alikuwapo hata kabla ya kuzaliwa na Mariamu; jambo hili pia Yesu Kristo kwa kinywa Chake Yeye mwenyewe ametuthibitishia alipokuwa akiwaambia Wayahudi kwamba:
Yeye aliye wa Mungu huyasikia maneno ya Mungu; hivyo ninyi hamsikii kwa sababu ninyi si wa Mungu.
Wayahudi wakajibu, wakamwambia, Je! Sisi hatusemi vema ya kwamba wewe u Msamaria, nawe una pepo?
Yesu akajibu, Mimi sina pepo; lakini Mimi namheshimu Baba yangu, na ninyi mwanivunjia heshima Yangu. Wala mimi siutafuti utukufu Wangu; Yuko mwenye kutafuta na kuhukumu. Amin, amin, nawaambia, Mtu akilishika neno langu, hataona mauti mileleBasi Wayahudi wakamwambia, Sasa tumeng’amua ya kuwa una pepo. Ibrahimu amekufa, na manabii wamekufa; nawe wasema, Mtu akuilishika neno langu, hataonja mauti milele. Wewe u mkuu kuliko baba yetu Ibrahimu, ambaye amekufa? Nao manabii wamekufa. Wajifanya u nani? Yesu akajibu, Nikijitukuza mwenyewe, utukufu wangu si kitu; anitukuzaye ni Baba Yangu, ambaye ninyi mwanena kuwa ni Mungu wenu. Wala ninyi hamkumjua; lakini mimi namjua. Nikisema ya kwamba simjui, nitakuwa mwongo kama ninyi; lakini namjua, na neno lake nalishika. Ibrahimu baba yenu, alishangilia kwa vile atakavyoiona siku yangu; naye akaiona, akafurahi.
Basi Wayahudi wakamwambia, Wewe haujapata bado miaka hamsini, nawe umemona Ibrahimu? Yesu akawaambia, Amin, amin, nawaambia, Yeye Ibrahimu asijakuwako, Mimi niko.” (Yohana 8:47-58)
Katika kisa tulichokisoma katika maandiko hayo (Yohana 8:47-57) tunajifunza mambo kadhaa hapo. Tumeona dhahiri jinsi ambavyo hata baadhi ya Wayahudi ilivyo wawia vigumu sana kumwelewa huyu Yesu ni nani; hata wakadiriki kusema kuwa Yesu anayo mapepo (mashetani). Hawakumwelewa kwa sababu walimtazama Yesu kibinadamu kama jinsi wao walivyo, lakini hawakujua kuwa Yesu ni alikuwepo hata kabla ya Yeye kuzaliwa na Mariamu. Huyo Ibrahimu anayeongelewa hapo ni yule ambaye habari zake tunazisoma katika kitabu cha MWANZO cha Biblia (Ibrahimu baba yake Isaka na Ishmaili). Wayahudi walishangaa; Inawezekanaje huyu Yesu aseme alimwona Ibrahimu aliyeishi na kufa miaka mingi tena zaidi ya elfu moja iliyopita, wakati huyu Yesu tumemwona utotoni mwake na hata sasa bado hajatimiza umri wa miaka hamsini? Hayo yalikuwa ni mawazo ya kibinadamu; tena inaezekana hata wewe ukawa ni miongoni mwa waliokuwa wanawaza hivyo; lakini, Yesu mwenyewe anatuthibitishia kwa kinywa Chake kwa kusema:
...Amin, amin, nawaambia, Yeye Ibrahimu asijakuwako, Mimi niko.” (Yohana 8:58)
Pia Yesu amewaambia Wayahudi kuwa huyo ambaye wao wanamwita Mungu (YEHOVA), Yeye ndiye Baba wa Yesu; tena Yesu anamjua ingawa hao Wayahudi hawamju (Yohana 8:54,55). Vile vile tusomapo kitabu cha MITHALI tunaona habari zinazo mhusu huyu Yesu; imeandikwa kwamba:
BWANA alikuwa nami katika mwanzo wa njia yake. Kabla ya matendo Yake ya kale. Nalitukuka tokea milele, tangu awali, Kabla haijawako dunia. Wakati visipokuwapo vilindi nalijidhihirisha... (...I was brought forth... – NKJV)...” (Mithali 8:22-24)
Usomapo Biblia ya Kiswahili; hapo nilipoandika “...Wakati visipokuwapo vilindi NALIJIDHIHIRISHA...” utaona baadhi ya Biblia za Kiswahili zimeandika “...NALIZALIWA...” lakini maana halisi hapo ni “...I was brought forth...” ambayo tafsiri yake ni “...NALIJITOKEZA...” au “...NALIJIDHIHIRISHA...
Kumbuka kuwa Wayahudi walimtambua Mungu kwa jina "YEHOVA" ambalo mara nyingi walitamka kwa kusema "BWANA." Hapo Biblia Takatifu inamtaja huyu Yesu likuwa pamoja na YEHOVA katika mwanzo wa njia za YEHOVA. Kabla ya YEHOVA kuumba cho chote (...matendo ya kale...) huyu Yesu alikuwepo. Hivyo basi; huyu Yesu alikuwapo “...tokea milele, tangu awali, Kabla haijawako dunia.” (Mithali 8:23) Neno “MILELE” maana yake ni wakati ambao hauna mwanzo wala mwisho; ni wakati usioweza kuhesabika.
Upo ushahidi mwingi sana ndani ya Biblia Takatifu unaotuthibitishia kuwa Yesu alikuwepo hata kabla ya kuumbwa kitu cho chote kile; kwani nao manabii pia walitabiri ujio wa Yesu ambaye alikuwepo tangu milele yote, na tena manabii hao walisema wazi wazi kuwa huyu Yesu ni Mungu. Unabii huo ni kama ifuatavyo:
ü       Yesu atazaliwa katika mji wa Bethlehemu.
Biblia Takatifu inasema kwamba:
Bali wewe, Bethlehemu Efrata, uliye mdogo kuwa miongoni mwa elfu za Yuda; kutoka kwako wewe atanitokea mmoja atakayekuwa mtawala katika Israeli; ambaye matokeo yake yamekuwa tangu zamani za kale, tangu milele.” (Mika 5:2)
Andiko hilo pia linamtaja Yesu kuwa: “...matokeo yake yamekuwa tangu zamani za kale, tangu milele.” (Mika 5:2)
ü       Yesu atazaliwa katika kabila la Yuda.
Biblia Takatifu inasema kwamba:
Fimbo ya enzi haitaondoka katika Yuda, Wala mfanya sheria kati ya miguu yake, Hata atakapokuja Yeye, mwenye milki, ambaye mataifa watamtii.” (Mwanzo 49:10)
Hapo tumeona panasema: “...Hata atakapokuja Yeye, mwenye milki...” ndio maana tukisoma kitabu cha YOHANA 1:10,11 tunaona pameandikwa kwamba: “Alikuwako ulimwenguni, hata kwa Yeye ulimwengu ulipata kuwako, wala ulimwengu haukumtambua. Alikuja Kwake, wala walio Wake hawakumpokea. Bali wote waliompokea aliwapa uwezo kufanyika watoto wa Mungu, ndio wale waliaminio jina Lake.” Yesu ndiye mwenye milki ya ulimwengu huu tunaouishi.
ü       Manabii walisema Yesu atazaliwa na bikira.
Biblia Takatifu inasema kwamba:
Kwa hiyo Bwana mwenyewe atawapa ishara: Tazama, bikira atachukua mimba, atazaa Mtoto mwanamume, naye atamwita jina Lake Imanueli.” (Isaya 7:14)
Jina “IMANUELI” maana yake ni “Mungu pamoja na wanadamu.
ü       Pia manabii walisema Yesu ni Mungu.
Biblia Takatifu inasema kwamba:
Maana kwa ajili yetu Mtoto amezaliwa, Tumepewa Mtoto mwanamume; Na uweza wa kifalme utakuwa begani Mwake; Naye ataitwa jina Lake, Mshauri wa ajabu, Mungu mwenye nguvu, Baba wa milele, Mfalme wa amani. Maongeo ya enzi yake na amani hayatakuwa na mwisho kamwe...” (Isaya 9:6,7)
Napo hapo pia tumeona panamtaja Yesu kuwa Yeye ni: “...Mungu mwenye nguvu...” na tena ufalme Wake ni wa milele yote na kamwe hautakuwa na mwisho.
Upo ushahidi mwingi sana ndani ya Biblia Takatifu unaotuthibitishia Uungu wa Yesu pamoja na umilele wa uwepo Wake wa tangu zamani hata baadae.
Sifa nyingine ya cheo cha Mungu ni hii ifuatayo:
B.     Yesu Kristo ameumba mbingu, nchi, watu, na ulimwengu wote.
Biblia Takatifu inatuambia kwamba:
...tuliumbwa katika Kristo Yesu...” (Waefeso 2:10)
Ni jambo lililo wazi kabisa kuwa sisi wanadamu wote pamoja na viumbe vyote ni kazi ya mikono ya Yesu. Yesu ameumba vitu vyote; tendo la mtu kuukana Uungu wa Yesu ni jambo la kumkosea heshima Mungu aliyekuumba. Ndio maana Yesu aliwaambia Wayahudi kwamba: “...ninyi mwanivunjia heshima Yangu...” (Yohana 8:49).
Tusomapo Biblia Takatifu katika kitabu cha YOHANA sura ya kwanza, tunaona pameandikwa:
Hapo mwanzo kulikuwako Neno, naye Neno alikuwako kwa Mungu, naye Neno alikuwa Mungu... Vyote vilifanyika kwa huyo; wala pasipo Yeye hakikufanyika cho chote kilichofanyika... Naye Neno alifanyika mwili, akakaa kwetu; nasi tukauona utukufu Wake, utukufu kama wa Mwana pekee atokaye kwa Baba; amejaa neema na kweli.” (Yohana 1:1,3,14)
Huyo “Neno” anayetajwa hapo ndiye Yesu Kristo. Mwandishi wa kitabu hicho cha YOHANA ametumia usemi wa: “...Neno alikuwako kwa Mungu...” akiwa anawafahamisha hususani Wayahudi waliokuwa wanajua kuwa YEHOVA ndiye Mungu wao. Kwa hiyo Yohana anasema “...Neno alikuako kwa Mungu...” kwa maana ya kwamba; huyu “...Yesu alikuwako kwa YEHOVA...ambaye wao Wayahudi walimtambua kuwa ndiye Mungu wao.
Pia zaidi tunaona Yohana anafafanua kwa kusema kuwa; huyu “...Yesu alikuwa Mungu...” Ufafanuzi zaidi tunauona katika YOHANA 1:14 ambapo Yohana amefafanua kwa kusema; “...Yesu alifanyika mwili; akakaa kwetu...” Biblia Takatifu inamtaja kwa wazi kabisa kuwa Yesu ni Mungu na ameumba vitu vyote “...Vyote vilifanyika kwa huyo; wala pasipo Yeye hakikufanyika cho chote kilichofanyika...” (Yohana 1:3).
Sifa nyingine ituthibitishiayo kuwa Yesu ni Mungu; ni hii ifuatayo:

C.     Yesu Kristo anayo amri na mamlaka ya kusamehe dhambi.
Kuna jambo lililowahi kutokea hadi likawashangaza watu; hebu fatilia kisa hiki. Biblia Takatifu inasema kwamba:
Wakaja watu wakimleta mtu mwenye kupooza, anachukuliwa na watu wanne. Na walipokuwa hawawezi kumkaribia (Yesu) kwa sababu ya makutano, waliitoboa dari pale alipokuwapo; na wakiisha kuivunja wakalitelemsha godoro alilolilalia yule mwenye kupooza. Naye Yesu, alipoiona imani yao, akamwambia yule mwenye kupooza, Mwanangu, umesamehewa dhambi zako. Na baadhi ya waandishi waliokuwako huko, wameketi, wakifikiri mioyoni mwao,
Mbona huyu anasema hivi? Anakufuru. Ni nani awezaye kusamehe dhambi isipokuwa mmoja, ndiye Mungu?
Mara Yesu akafahamu rohoni mwake kwamba wanafikiri hivyo nafsini mwao, akawaambia, Mbona mnafikiri hivi mioyoni mwenu? Vyepesi ni vipi, kumwambia mwenye kupooza, Umesamehewa dhambi zako, au kusema, Ondoka, ujitwike godoro lako, uende?
Lakini mpate kujua ya kwamba Mwana wa Adamu anayo amri duniani ya kusamehe dhambi – Akamwambia yule mwenye kupooza,
Nakuambia, Ondoka, ujitwike godoro lako uende nyumbani kwako.
Mara akaondoka, akajitwika godoro lake, akatoka mbele yao wote; hata wakastajabu wote, wakamtukuza Mungu, wakisema, Namna hii hatujapata kuiona kamwe.” (Marko 2:3-12)
Kwa Wayahudi uponyaji haukuwa kitu kigeni kwao kwani hata manabii enzi za Agano la Kale nao walitumia nguvu za Mungu kuponya wagonjwa; lakini, jambo lililoonekana geni kwa Wayahudi ni kusikia Yesu amesema “...Umesamehewa dhambi zako...” (Marko 2:5) Kauli hiyo ya Yesu iliwafanya waone kwamba Yesu AMEKUFURU kwa maana mwenye mamlaka ya kusamehe dhambi ni Mungu pekee. Watu hao walidhani Yesu amekufuru kwa sababu hawakujua kuwa Yesu ni Mungu ingawa alikuwa ameuvaa mwili wa kibinadamu kama sisi.
Ukimpokea Yesu; anakusamehe dhambi zako zote. Haijalishi umetenda dhambi nyingi kiasi gani; haijalishi hali uliyonayo hivi sasa. Fahamu kwamba Yesu anakupenda. Neno la Mungu linasema kwamba:
...asema BWANA. Dhambi zenu zijapokuwa nyekundu sana, zitakuwa nyeupe kama theluji...” (Isaya 1:18)
Yesu ni Mungu, endapo ukimpokea atakusamehe dhambi zote ulizozitenda. Yesu anakupenda sana. Hebu leo mpe Yesu maisha yako ayatawale; Yesu ataiondoa kiu hiyo ya kutenda dhambi ikufanyayo ushindwe kujizuia kuwaka tamaa mbaya za mwili wako; Yesu atakupatia ulinzi ambao utazuia pepo wachafu wasiingilie maisha yako; Yesu atakubariki na kufungua tumbo lako lililokosa mtoto kwa muda mrefu wote huo unaotaabika hata sasa; Yesu atawarejesha kwako watoto wako ambao wamekataa kukutii hata wametoweka kwako; Yesu atakupatia uzima na kuyaondoa magonjwa yote hayo yanayokutesa hata sasa; Yesu atakubariki na kukupatia uzima wa milele.
Kwa kweli nashindwa kuuelezea kwa ufasaha zaidi upendo wa Yesu juu yako kwa maana wewe ni wathamani kubwa sana mbele za Mungu. Mimi nachoweza kukwambia ni kwamba: Yesu anakupenda tena hataki upotee. Mpe Yesu maisha yako sasa ili ufurahie uzuri wa pendo Lake.
Jambo jingine lituthibitishialo kuwa Yesu ni Mungu; ni hili lifuatalo:
D.     Yesu Kristo Ndiye atanayekuja kuuhukumu ulimwengu wote siku ya kiyama.
Jambo hili si mzaha wala uzushi bali ni kweli; Yesu Kristo anakuja kuhukumu ulimwengu wote. Yesu Kristo ametutamkia kwa kiywa Chake kwa kusema kwamba;
Tena Baba hamhukumu mtu ye yote, bali amempa Mwana hukumu yote; ili watu wote wamheshimu Mwana kama vile wanavyomheshimu Baba.” (Yohana 5:22,23)
Katika hukumu siku ya kiyama hatutegemei kumwona YEHOVA akija kuhukumu ulimwengu, bali, Yesu Kristo ndiye ajaye kuhukumu ulimwengu. Hii itakuwa hivyo ili WATU WOTE WAMHESHIMU Yesu sawa sawa na jinsi ambavyo wanamheshimu YEHOVA. Hapo ndipo viumbe vyote watathibitisha kuwa Yesu ni Mungu. Biblia Takatifu inasema kwamba:
...kwa jina la Yesu kila goti lipigwe, la vitu vya mbinguni, na vya duniani, na vya chini ya nchi; kila ulimi ukiri ya kuwa YESU KRISTO NI BWANA...” (Wafilipi 2:10,11)
Hakika Yesu ni Mungu. Najua hapa huwachanganya baadhi ya watu hata wanaweza kuhoji;
Je! Wapo Miungu wangapi? Kwa maana tunasikia habari za Mungu Baba, Mungu Mwana, na Mungu Roho Mtakatifu? Inawezekanaje tuseme Yupo Mungu mmoja wakati hapo tunaona wapo watatu?
Ni kweli Utatu Mtakatifu wa Mungu umekuwa mgumu sana kueleweka kwa watu wengi kutokana na mafundisho dhaifu waliyoyapokea kutoka kwa viongozi wao wa madhehebu yao na imani zao. Je! Utatu Mtakatifu wa Mungu ni uzushi uliotungwa na wanadamu kwa lengo la kupotosha watu au Biblia Takatifu inatuthibitishia wazi wazi kuhusu Utatu Mtakatifu wa Mungu? Hebu twende katika neno la Mungu tuone jinsi lisemavyo.
Biblia Takatifu inatuambia kwamba:
Kwa maana wako watatu washuhudiao mbinguni: Baba, Neno, na Roho Mtakatifu; na watatu hawa ni umoja.” (1 Yohana 5:8 / 1 John 5:7)
Andiko hilo katika Biblia ya New King James Version inasema “...these three are one.” (1 John 5:7) kwa maana ya kwamba “...WATATU HAWA NI MMOJA.” Hebu tujiulize; je! Huo umoja wao unaowafanya watatu hao (YEHOVA, Yesu, na Roho Mtakatifu) hata wote wawe MMOJA ni upi?
Umoja wao upo katika Uungu. Wote watatu wanaungana kuwa Mungu mmoja kwa maana ya kwamba uumbaji wa vitu vyote umefanywa kwa pamoja na hawa watatu (yaani; YEHOVA, Yesu, pamoja na Roho Mtakatifu).
Tukirejea katika uumbaji; Neno la Mungu linasema kwamba:
Mungu akasema, Na Tumfanye mtu kwa mfano Wetu, kwa sura Yetu...” (Mwanzo 1:26)
Pindi niliposoma andiko hilo kwa umakini nilijiuliza; Mbona Mungu hakusema;

"...Nimfanye mtu kwa mfano Wangu, kwa sura Yangu..."? Kwa nini Mungu ametumia maneno "...kwa mfano WETU, kwa sura YETU..."? Maneno hayo "...WETU..." na "...YETU..." yanadhihirisha hapo kuna zaidi ya mmoja. Je, ni nani mwingine aliye muumba mwanadamu zaidi ya Mungu?

Wakati nikiwa ninajiuliza maswali mengi, ndipo Roho Mtakatifu akanifundisha kwamba neno "Mungu" ni cheo, na sifa zake ndizo tulizojifunza hapo awali. Mungu hufanya kazi katika ushirika ambao katika Umoja huo ndipo aliumba vitu vyote.
Yesu anakupenda, mpe maisha yako sasa ili akuokoe. Ni jambo la imani tu, ukiamini ndani ya roho yako na kumkiri Yesu kwa dhati kwa kinywa chako; hakika hapo hapo unakuwa umeokoka.
Kumpokea Yesu maishani mwako maana yake ni kukiri kwamba Yesu ni Bwana, Yesu ni Mungu, pamoja na KUKIRI kwamba Yesu pekee ndiye uzima wa milele wala hakuna kiumbe ye yote yule awezaye kuokoa isipokuwa Yesu pekee ambaye ni Mungu wetu.
Inawezekana kabisa ya kuwa wewe unayesoma ujumbe huu hujaokoka - yaani hujampokea Yesu Kristo ndani ya roho yako kuwa Bwana na Mwokozi wako; Lakini sasa umeona umuhimu wa kumpokea Yesu Kristo katika maisha yako.
Naamini Roho Mtakatifu ameweka fursa hii mikononi mwako kwa mpango maalumu wa Mungu ili ufike mahali pa kutubu na kuokoka. Wokovu ni kwa ajili ya uponyaji wako ili uwe na uzima wa milele; kamwe usimtazame huyo aliye pembeni mwako kwamba akisikia umeokoka atachukia; wala usiisikilize hiyo sauti ikwambiayo ndani ya akili zako kwamba "subiri" Hiyo ni sauti itokayo kwa yule mwovu Shetani ambaye anataka wewe ufe katika dhambi zako. Fahamu kwamba uzima wako wa milele unauandaa sasa; pia Biblia inasema hakuna neema baada ya kifo; kwa maana imeandikwa:
Na kama vile watu walivyowekewa kufa mara moja, na baada ya kufa hukumu.”  (Waebrania 9:27)
Mtu akifa kinachofuata ni hukumu. Asije akatokea mtu akakudanganya kwamba yapo maombi yanayoweza kuwaombea wafu nao wakasamehewa dhambi zao (mwulize mtu huyo akwambiae hivyo; mwambie akuonyeshe andiko ndani ya Biblia Takatifu linalosema unaweza kumwombea mfu.) Huo ni uongo tena utokao kwa Shetani. Neno la Mungu linasema kwamba:
Yeye si Mungu wa wafu, bali wa walio hai. Hivyo mwapotea sana.” (Marko 12:27)
Nakushauri usiiache neema hii ya wokovu iliyopo mbele yako sasa ikipite. Wakati huu ni wa thamani sana kwako kwa maana huijui kesho wala badae ikoje. Tafakari kwa kina kati yako wewe na Mungu ni nani anahitaji msaada wa mwenzake. Tubu sasa. Sikulazimishi ila fanya sawa na kile Mungu anachoshuhudia ndani ya roho yako. Fahamu kuwa; haiwezekani kuona baraka za Damu ya Yesu bila ya wewe kuokoka.
Kama unataka kuokoka sasa hivi; Tafuta mahali palipo na utulivu, na usome kwa kutamka kwa kinywa chako sala ifuatayo: (ukiweza unaweza kupiga magoti unapoomba sala hii)
 “Ee Mungu wangu ulie Mtakatifu. Ninakuja mbele zako. Mimi ni mwenye dhambi. Naomba unisamehe dhambi zangu zote nilizokukosea katika maisha yangu yote. Ninatubu kwa dhati ya kweli kutoka rohoni mwangu. Naomba damu ya Yesu Kristo iliyomwagika msalabani kwa ajili yangu initakase sasa katika roho yangu na nafsi yangu na mwili wangu. Nimefungua moyo wangu. Bwana Yesu Kristo nakukaribisha ndani yangu. Ingia kwa uwezo wa Roho Wako – Uwe Bwana na Mwokozi wangu kuanzia sasa na siku zote. Nakuomba unifanye niwe vile utakavyo mimi niwe. Ahsante kwa kunisamehe na kwa kuniokoa. Nimejitoa kwako nikutumikie katika siku zote za maisha yangu. Shetani hana mamlaka tena juu yangu katika jina la Yesu Kristo. Amina."
Ikiwa umesoma sala hii kwa kukusudia kabisa na kwa imani, basi wewe umeokoka na dhambi zako zote zimesamehewa kabisa. Damu ya Yesu iko juu yako sasa.
Baada ya kuokoka
Unapoanza maisha haya mapya katika Yesu Kristo nakushauri mambo yafuatayo:
(a)         Zungumza na Mungu kwa maombi kila siku (Yohana 15:7).

(b)         Soma Neno la Mungu (Biblia) kila siku (Matendo ya Mitume 17:11).

(c)         Mruhusu Roho Mtakatifu akutawale (Wagalatia 5:16-25; Warumi 8:14-17).

(d)         Umtumaini Mungu kwa kila jambo katika maisha yako (1Petro 5:7; Zekaria 4:6).

(e)         Usiache kukusanyika na kushirikiana na wengine waliompokea Yesu Kristo kuwa Mwokozi wao ili uimarike zaidi (Waebrania 10:25).

(f)          Ikemee dhambi na ujitenge nayo. Ukiamini, kwa jina la Yesu unaweza kuishi maisha matakatifu (Yakobo 4:7-8).

(g)         Jidhihirishe wazi kwa watu kwamba wewe umeokoka na pia shuhudia kwa watu injili (Mathayo 10:32-33; Warumi 1:16).

Hongera kwa kuokoka, tangu sasa umekuwa kiumbe kipya. Nakutakia baraka tele katika jina la Yesu Kristo, amina.

Ni mimi mtumishi wa Mungu,

              Mwinjilisti Masanja Sabbi.

TUMA KWA RAFIKI :

Twitter FacebookMore

 
Kuhusu Huduma Hii | Masharti Ya Utumiaji Wa Tovuti Hii | Wasiliana Nasi | Tangaza Kupitia Tovuti Hii