Tuesday, June 18, 2013

HAKUNA DHAMBI KUBWA WALA DHAMBI NDOGO.

WAPENZI MSIDANGANYIKE ! ! !


HAKUNA DHAMBI KUBWA WALA DHAMBI NDOGO.

DHAMBI NI DHAMBI TU. DHAMBI ZOTE HUKUMU YAKE NI KATIKA ZIWA LA MOTO WA MILELE.

Neno la Mungu linatuambia kwamba:

"Bali waoga, na wasioamini, na wachukizao, na wauaji, na wazinzi, na wachawi, na hao waabuduo sanamu, na waongo wote, sehemu yao ni katika lile ziwa liwakalo moto na kiberiti." - UFUNUO 21:8

HAKUNA DHAMBI KUBWA WALA DHAMBI NDOGO.

Wapo watu wanaofarijiana kwa kudhani ipo dhambi kubwa na pia ipo ndogo; Kwa akili zao za kibinadamu wanazipa dhambi uzito kulingana jinsi wao zinavyowagusa. Wapo watu hudhani kuwa adhabu ya dhambi ya kusema uongo ni tofauti na ya dhambi ya kuua. Jambo hili limefanya watu waone dhambi ya uongo haina uzito sana hata wamekuwa na desturi ya kusema uongo bila hata kujuta wala kutubu; Shetani amewafanya waizoelee dhambi. Bila shaka si jambo geni kwako kumsikia mtu anapigiwa simu alafu anamjibu yule aliyempigia kuwa: "NIPE DAKIA MOJA TU, NITAKUWA NIMEFIKA HAPO.Mtu huyo anasema hivyo wakati yupo umbali ambao kwa hakika hawezi kufika mahali hapo hata kwa kutumia nusu saa, lakini amesema kwa lengo la kumridhisha tu huyo anayemwitaji.
Pia yawezekana si jambo geni kwako kusikia mtu amepigiwa simu na kuulizwa: "UPO WAPI?" naye akajibu: "NIPO NYUMBANI." wakati mtu huyo hayupo nyumbani na yawezekana yupo matembezini na wala hana mpango wa kurudi nyumbani kwa muda huo. Huu ni mfano mdogo sana wa uongo uliozoeleka na kuonekana kuwa kitu cha kawaida sana. Wapo watu wanaodhani uzinzi na uuaji ni dhambi kubwa sana kuliko uongo hata wamediriki kuwatenga wazinzi na kuwakumbatia waongo, tena wanakula nao na kufurahi pamoja. Je! Macho ya Mungu yanaitazamaje dhambi?
Neno la Mungu linasema kwamba:

"...Usipotenda vyema dhambi iko, inakuotea mlangoni nayo inakutamani wewe, walakini yakupasa uishinde." - MWANZO 4:7.

Mungu anasema "...Usipotenda vyema dhambi iko..." Kwa maana ya kwamba kila kitu kisicho chema mbele za macho ya Mungu ni dhambi. Kwa Mungu dhambi ni dhambi na kila aitendaye dhambi kwa kufahamu asipotubu inampasa hukumu. Je! Nini maana ya neno dhambi?

DHAMBI:
Dhambi ni kutenda kinyume na mapenzi ya Mungu kwa kujua (kwa makusudi) ama kwa kutojua. Kila kitu ambacho si chema mbele za Mungu hicho ni dhambi. Dhambi ni kufanya kitu kilicho chukizo mbele za Mungu. Biblia Takatifu inatuambia kwamba: Kila lisilo la haki ni dhambi...” – 1 Yoh 5:17 Tunapaswa tuwe makini sana tusomapo neno la Mungu; hapo Biblia Takatifu inaposema: Kila lisilo la haki ni dhambi... Neno "KILA" maana yake ni "YOTE" Tunapozungumzia neno DHAMBI tunapaswa kulitazama neno hili kwa upana zaidi. Zipo dhambi nyingi wazifanyazo watu pasipo wao kujua; mf. hata KUTOKUAMINI ni DHAMBI. Na hao ambao hawakuamini inawapasa hukumu ya adhabu. Neno la Mungu linasema kwamba:

"Na wakati alipowatuma BWANA kutoka Kadesh-barnea, akawaambia, Kweeni mkaimiliki nchi niliyowapa; ndipo mkaasi juu ya maagizo ya BWANA, Mungu wenu, hamkusadiki wala hamkusikiza sauti Yake." - KUMB 9:23.

Hapo tunaowa watu hao wana wa Israeli HAWAKUMSADIKI HAWAKUMWAMINI Mungu na wala hawakutii (hawakusikiliza) sauti Yake. Kwa dhambi hiyo ya KUTOAMINI / KUTOSADIKI neno na maagizo ya Mungu tunaona Biblia inasema: "...BWANA alisema atawaangamiza." - KUMBU 9:25. Dhambi hiyo tu ilitosha kabisa kwa Mungu kutoa adhabu ya kuwaangamiza (kuwaua) watu hao. Kibinadamu yawezekana jambo hili lisiingie akilini lakini kwa uhalisi hivyo ndivyo Mungu alivyo; Kwake hakuna dhambi kubwa wala ndogo, dhambi ni dhambi tu. KUTOAMINI ni DHAMBI. Bwana Yesu anasema kwa watu wasioamini kwamba:

"...mtakufa katika dhambi zenu; kwa sababu msiposadiki ya kuwa Mimi ndiye, mtakufa katika dhambi zenu." - YOHANA 8:24.

KUTOAMINI / KUTOSADIKI ni dhambi kwa sababu ni tendo la kukosa nidhamu kwa kuukataa ukweli ambao Mungu ameudhihirisha. Kila asiyeamini neno la Mungu, na kila anayeasi maagizo ya Mungu kwa makusudi anastahili adhabu pasipo kujali ni agizo lipi au mangapi (mengi au moja) amevunja. Adhabu ipo juu ya kila atendaye dhambi. Neno la Mungu linasema kwamba:

"Aaminiye yeye haukumiwi; asiyeamini amekwisha kuhukumiwa..." - YOHANA 3:18.

Tendo la KUTOAMINI neno la Mungu hapo hapo tayari unakuwa umeandikiwa adhabu (usipotubu na kuamini adhabu inakungoja). Mungu huyatazama machukizo yote kuwa ni kitu kisichofaa mbele Zake. Kwa Mungu hakuna dhambi kubwa wala dhambi ndogo kwa maana hukumu ya watenda dhambi wote ni katika ziwa la moto wa mateso ya milele (UFUNUO 21:8).

Sasa basi; Dhambi imegawanyika katika makundi makuu mawili. Biblia Takatifu inafafanua kwa kusema kwamba:

Kila lisilo la haki ni dhambi, na iko dhambi isiyo ya mauti.” – 1 Yoh 5:17.

Hapo tunaona Biblia Takatifu inasema: "....na iko dhambi isiyo ya mauti.” Je! Nini maana ya andiko hilo?

TOFAUTI KATI YA DHAMBI YA MAUTI NA DHAMBI ISIYO YA MAUTI:

1. - DHAMBI YA MAUTI.

Dhambi ya mauti ni kila dhambi aifanyayo mwanadamu kwa kukusudia. Hapa namaanisha kwamba; Dhambi ya mauti hutokea pale mtu amepanga kabisa kuvunja sheria ya Mungu. Yawezekana mtu akatamani simu ya mwenzake, baada ya kutamani akaamua kufanya mikakati ya kuiiba, akamvizia na kuiiba simu hiyo, kisha akatoweka nayo. Dhambi ya namna hiyo inaitwa ni dhambi ya mauti kwa sababu kumekuwa na mlolongo wa utekelezaji wa dhambi hiyo. Au, mwanamume akamtongoza mwanamke asiye mkewe, kisha wakakubaliana kukutana mahali kwa ajili ya uzinzi / uasherati, na wakatekeleza adhma yao kwa kile walicho kusudia. Dhambi ya namna hiyo pia inaitwa ni dhambi ya mauti kwa sababu kumekuwa na mlolongo wa utekelezaji wa dhambi hiyo; na tena yawezekana Roho Mtakatifu amekushuhudia rohoni mwako kwa kukuonya lakini wewe ukakaidi na ukafanya kile ulicho kusudia. Kila dhambi ya makusudi inaitwa ni DHAMBI YA MAUTI. Kwa nini basi iitwe DHAMBI YA MAUTI? - Ni kwa sababu umetenda dhambi ukiwa unafahamu kabisa utendalo, na tena Roho Mtakatifu amekuonya rohoni mwako au kwa njia ya watu mbali mbali lakini wewe ukakaidi kutii. Dhambi hiyo ni ya mauti kwa sababu unajua ufanyalo; na mshahara wa dhambi ni mauti.

2. – DHAMBI ISIYO YA MAUTI.

Hii hutokea pale mtu atendapo dhambi pasipo kujua (yaani hajui afanyalo). Yawezekana mtu akatenda dhambi na bado asijue kama ametenda dhambi; mtu huyo katenda dhambi si kwa kusudi bali hajui afanyalo. Dhambi hiyo ndiyo inaitwa isiyo ya mauti.

Dhambi ya mauti huwa na gharama, ni lazima yeye aliyeitenda atubu yeye mwenyewe; bali dhambi isiyo ya mauti inaweza ikasamehewa kwa njia ya maombi ya mtu mwingine (yaani, mtu anaweza kuombewa na mtu mwingine naye akasamehewa). Biblia Takatifu inasema kwamba:

Mtu akimwona ndugu yake anatenda dhambi isiyo ya mauti, ataomba, na Mungu atampa uzima kwa ajili ya hao watendao dhambi isiyo ya mauti.” – 1 Yoh 5:16

Maana ya andiko hilo ni hii: Unaweza kumwona mtu (ndugu yako / aliye okoka) ametenda dhambi pasipo yeye kujijua kama ametenda dhambi; mf. Amefundisha neno fulani kimakosa pasipo yeye kujitambua; au kafanya dhambi ambayo hajajua kama anakosea (yawezekana ameokoka lakini bado ni mchanga kiroho) mtu wa namna hiyo unaweza kumwombea naye Mungu akamsamehe na kumpatia uzima (yaani Mungu akamwimarisha) tena; ndiyo maana katika andiko hilo tunaona panasema:

...ataomba, na Mungu atampa uzima kwa ajili ya hao watendao dhambi isiyo ya mauti.

Hiyo ndiyo maana ya andiko hiloVile vile mtu afanyapo dhambi bila kutambua, alafu baadae akaambiwa kuwa amekosa, mtu huyo anapaswa kutubu kwa dhambi ile aliyokuwa ameitenda hapo awali bila kujua. Na Biblia Takatifu inatuambia kwamba:

"...kutakuwa na furaha mbinguni kwa ajili ya mwenye dhambi mmoja atubuye..." - Luka 15:7.

Mtu aliyetenda dhambi bila yeye kujua kuwa anatenda dhambi, pindi tu anapotambua kuwa alitenda dhambi anapaswa kutubu papo hapo.
Tukija kwenye upande wa dhambi ya mauti; Dhambi hii nayo husameheka kwa njia ya toba. Biblia  Takatifu inatuambia kila ulifanyalo na Roho Mtakatifu akashuhudia rohoni mwako kuwa umefanya hatia, hiyo ni dhambi; Ni dhambi kwa kwa sababu umeonywa na Mungu lakini wewe ukakaidi sauti Yake. Hata kama ikatokea umetenda dhambi, Biblia Takatifu inatuambia kwamba tunaye Mpatanishi wetu ambaye ni Yesu. Biblia inasema:

...Na kama mtu akitenda dhambi tunaye Mwombezi kwa Baba, Yesu Kristo mwenye haki, naye ndiye kipatanisho kwa dhambi zetu; wala si kwa dhambi zetu tu, bali kwa dhambi za ulimwengu wote.” -1 Yoh 2:1-2

Biblia inaposema “...NA KAMA MTU AKITENDA DHAMBI...” neno “...KAMA...” linamaanisha; ENDAPO IKATOKEA MTU AKATENDA DHAMBI; mtu huyo anapaswa kutubu kwa kuwa Yupo Yesu ambaye ni Mpatanishi wetu kwa kutuondolea dhambi: "...naye ndiye kipatanisho kwa dhambi zetu...” Biblia inaposema “...DHAMBI ZETU..." hapo inatuzungumzia sisi tuijuayo kweli. Na si hivyo tu; bali huyu Yesu ni mpatanishi wa “...DHAMBI ZA ULIMWENGU WOTE." yaani wale wasioijua kweli nao wanasamehewa kwa njia ya Yesu endapo nao wakitubu na kumpokea Yesu awatawale.
Japokuwa tunaye Mpatanishi kwa ajili ya dhambi zetu, lakini Mungu hajatupa ruhusa ya kutenda dhambi kwa makusudi, kwa sababu kila mtu atendaye dhambi huyo ni wa Ibilisi (Shetani) kwa maana imeandikwa:

"Atendaye dhambi ni wa Ibilisi..." - 1 Yoh 3:8.

Mtu huyo akifa pasipo kutubu, moja kwa moja hukumu yake ni kutupwa katika ziwa la moto wa mateso ya milele kwa maana hakuna neema wala msamaha wa dhambi kwa wafu (WAEBRANIA 9:27). Wokovu si mwisho wa vita dhidi ya Shetani bali ndio mwendelezo wa vita hivyo. Shetani hamwangushi mtu aliyeanguka bali hufanya mbinu za kumwangusha yule aliyesimama. Shetani anataka watu waanguke dhambini. Pindi utendapo dhambi tu wewe unakuwa wa Ibilisi hata kama ulikuwa umeokoka. Japokuwa majaribu tunayo mengi; tamaa zinatupata nyingi; lakini tunapaswa kujilinda, na endapo ikitokea mtu akaanguka dhambini basi anapaswa kutubu kwa ajili ya kujitakasa. Biblia inatuambia kwamba:

Tukisema hatuna dhambi, twajidanganya wenyewe, wala kweli haimo mwetu. Tukiziungama dhambi zetu, Yeye ni mwaminifu na wa haki atuondolee dhambi zetu, na kutusafisha na udhalimu wote.” – 1 Yoh 1:8-9.

Zipo dhambi nyingi sana watendazo watu pasipo kufahamu, kwani hata tamaa mbaya ni dhambiTunapaswa kujenga desturi ya kutubu dhambi kila wakati. Bwana Yesu anatuambia kwamba:

"...Kila mtu atazamaye mwanamke kwa kumtamani, amekwisha kuzini naye moyoni mwake. Jicho lako la kuume likikukosesha, ling'oe ulitupe mbali nawe; kwa maana yakufaa kiungo chako kimoja kipotee wala mwili wako mzima usitupwe katika jehanum." - Mathayo 5:28-29.

Hapo Yesu hajazungumza kwa fumbo wala kwa mfano; bali hapo anamaanisha ni afadhali kwako KULING'OA (kuliondoa kabisa) jicho lako ambalo limekufanya utamani. Huo si mfano bali amesema kwa uhalisi kabisa. Yawezekana Shetani akapanda mawazo akilini mwako nawe ukajikuta umetamani kitu; au, yawezekana mbele ya macho yako kikapita kitu ambacho kikafanya mwili wako uingiwe na tamaa mbaya. Tamaa hiyo mbaya ni dhambi na unalazimika utubu. Endapo usipotubu utakuwa umeonyesha ukaidi na dhambi hiyo itahesabiwa ni dhambi ya mauti kwako; hapo utakuwa ni sawa na yule aliyefanya dhambi kwa makusudi. Bwana Yesu amesema:"...Kila mtu atazamaye mwanamke kwa kumtamani, amekwisha kuzini naye moyoni mwake." Kitendo cha kumtamani kwa macho tu mwanamke tayari unakuwa umezini naye hata kama haujamtongoza wala kumwingilia kimwili. Mungu huihesabu hiyo tamaa kuwa ni dhambi; Hivyo unapaswa kutubu. Dhambi hiyo ya tamaa inatosha kabisa kwa Mungu kumwadhibu mtu huyo kwa kumpa hukumu ya jehanum milele. Kibinadamu jambo hili linaweza lisikuingie akilini lakini huu ndio ukweli ulivyo. Kila mtu afanyaye dhambi kwa kufahamu (kwa kutambuainampasa hukumu ya adhabu bila kujalisha ukubwa wala udogo wa dhambi hiyo. Tunapogundua tumetenda dhambi tunapaswa KUTUBU.  Neno TOBA maana yake ni kumrudia Mungu. Biblia inaposema: “...TUKIZIUNGAMA DHAMBI ZETU...” neno UNGAMA maana yake ni KUKUBALI au KUKIRI ya kuwa wewe ni mkosaji na unajuta na kuhitaji msamaha na msaada wa Mungu. Ndipo Biblia inatuambia: “...Yeye ni mwaminifu na wa haki atuondolee dhambi zetu, na kutusafisha na udhalimu wote.” – 1 Yoh 1:8-9.
Watu hukosea kuzipima dhambi uzito. DHAMBI NI DHAMBI TU. HAKUNA DHAMBI KUBWA WALA DHAMBI NDOGO. Biblia Takatifu inapotuambia:

Kila lisilo la haki ni dhambi, na iko dhambi isiyo ya mauti.” – 1 Yoh 5:17

Maana ya andiko hilo ni hii: Kila lisilo la haki ni dhambi isipokuwa kama umetenda pasipo kufahamu. Kutenda pasipo kujua huko ndiko kunaitwa dhambi isiyo ya mauti. Lakini endapo mtu akisema uongo kwa kukusudia basi hapo ajue kuwa ametenda dhambi ya mauti. Ndiyo maana Biblia inatuambia: “Kila atendaye dhambi, afanya uasi; kwa kuwa dhambi ni uasi.” - (1 Yon 3:4). Ni makosa sana kuzipa vipimo vya uzito dhambi za makusudi. Biblia Takatifu inatuambia kwamba:

Maana mtu awaye yote atakayeishika sheria yote, ila akajikwaa katika neno moja, amekosa juu ya yote. Kwa maana Yeye aliyesema, Usizini, pia alisema, Usiue. Basi ijapokuwa hukuzini, lakini umeua, umekuwa mvunja sheria.” – Yakobo 2:10-11.

Kila avunjaye sheria ya Mungu (kwa kufahamu) hukumu yake ni katika jehanum ya moto; awe ni mwizi, mwongo, mwuaji, msengenyaji, mtukanaji, mwenye mizaha, mzinzi, asiyeamini, mwabudu sanamu, n.k. wote hukumu yao ni katika ziwa la moto wa mateso ya milele (Ufunuo 21:8).
Kila atendaye dhambi ni wa Shetani (1 Yoh 3:8) lakini endapo ukitubu unakuwa tena mtakatifu; ndiyo maana Mungu anapendezwa na watakatifu watuliomo duniani. Ukiwa upande wa Mungu unapaswa kujilinda. Unapojilinda unakuwa wewe ni wa Mungu kwa maana aliye wa Mungu HATENDI DHAMBI. Biblia Takatifu inasema:

"Wapenzi, sasa tu wana wa Mungu, wala haijadhihirika bado tutakavyokuwa; lakini twajua ya kuwa atakapodhihirishwa, tutafanana na Yeye; kwa maana tutamwona kama alivyo. Na kila mwenye matumaini haya katika Yeye hujitakasa, kama Yeye alivyo mtakatifu. Kila atendaye dhambi, afanya uasi; kwa kuwa dhambi ni uasi. Nanyi mnajua ya kuwa Yeye alidhihirishwa, ili aziondoe dhambi; na dhambi haimo ndani Yake. Kila akaaye ndani Yake hatendi dhambikila atendaye dhambi hakumwona Yeye, wala hakumtambua... mtu na asiwadanganye; atendaye haki yuna haki, kama Yeye alivyo na haki; atendaye dhambi ni wa Ibilisikwa kuwa Ibilisi hutenda dhambi tangu mwanzoKwa kusudi hili Mwana wa Mungu alidhihirishwa, ili azivunje kazi za Ibilisi. Kila mtu aliyezaliwa na Mungu hatendi dhambi, kwa sababu uzoa Wake wakaa ndani yake; wala hawezi kutenda dhambi kwa sababu amezaliwa kutokana na Mungu. Katika hili watoto wa Mungu ni dhahiri, na watoto wa Ibilisi nao. Mtu ye yote asiyetenda haki hatokani na Mungu, wala yeye asiyempenda ndugu yake... Sisi tunajua ya kuwa tumepita toka mautini kuingia uzimani, kwa maana twawapenda ndugu. Yeye asiyependa, akaa mautini. Kila amchukiaye ndugu yake ni mwuaji; nanyi mnajua ya kuwa kila mwuaji hana uzima wa milele ukikaa ndani yake... tusipende kwa neno, wala kwa ulimi, bali kwa tendo na kweli. Katika hili tutafahamu ya kwamba tu wa kweli, nasi tutaituliza mioyo yetu mbele Zake, ikiwa mioyo inatuhukumu; kwa maana Mungu ni mkuu kuliko mioyo yetu naye anajua yote. Wapenzi, mioyo yetu isipotuhukumu, tuna ujasiri kwa Mungu; na lo lote tuombalo, twalipokea Kwake, kwa kuwa twazishika amri Zake, na kuyatenda yapendezayo machoni Pake..." - 1 Yoh 3:2-22.

Katika hayo yakupasa kuyachunguza maisha yako; bila shaka unahitaji toba. Tubu sasa kwa maana hakuna neema baada ya kifo. Mungu anakupenda, tubu sasa. Bwana Yesu anasema kwamba: "...Kila dhambi na kila neno la kufuru watasamehewa wanadamu, ila kwa kumkufuru Roho Mtakatifu hawatasamehewa." - (Mathayo 12:31). Ni dhambi moja tu asiyosamehewa mwanadamu. Je! Wajua maana ya KUMKUFURU ROHO MTAKATIFU? Bonyeza hapa ujifunze somo hili zuri, hakika utabarikiwa.
Nakutakia baraka na mafanikio mema. Mwenyezi Mungu akulinde na afungue fahamu zako na macho ya rohoni mwako ili uione kweli, uijue kweli na uifuate kweli katika jina la Yesu Kristo. Amina.

Ni mimi Mtumishi wa Mungu,

             Mwinjilisti Masanja Sabbi.

1 MAONI:

Gift G, kawiche said...

Ubarikiwe sana Mtumishi W a Kristo Yesu

Post a Comment

TUMA KWA RAFIKI :

Twitter FacebookMore

 
Kuhusu Huduma Hii | Masharti Ya Utumiaji Wa Tovuti Hii | Wasiliana Nasi | Tangaza Kupitia Tovuti Hii