Sunday, January 28, 2018

BWANA, TUFUNDISHE SISI KUSALI (Luka 11:1)


SALA / MAOMBI
Hili ni tendo ambalo watu wanaoamini humwendea Mungu wakimwabudu, wakifanya toba, wakimshukuru na kumwomba mambo mbali mbali. Sala / Maombi ni mawasiliano ya moja kwa moja kati ya mtu anayeamini na Mungu. Unamweleza Mungu kile kilichomo ndani yako (hatuombi kwa kukariri bali tunasema kile kilichomo ndani yetu); yanaweza kuwa ni sala / maombi binafsi au maombezi kwa ajili ya wengine.

Tunaposoma Biblia katika Injili ya Luka 11:1, mwanafunzi wa Yesu anamwambia Bwana wake kwamba:

“…Bwana, tufundishe sisi kusali…” – Luka 11:1

Kuna jambo la kuzingatia hapa: Kabla ya kuingia katika maombi, ni muhimu sana kutambua kwanini tunaomba, ni nani tunapaswa kumwomba, na kwanini tumwombe yeye; baada ya kufahamu hivyo, hapo ndipo tuingie katika maombi.

1. Tunaomba kwa sababu sisi ni dhaifu, hatujitoshelezi pasipo msaada wa kiroho. Tunahitaji dira, mwongozo na usimamizi ili tuweze kutenda vema. Pia tunasali kwa ajili ya kurudisha shukrani kwa Yeye atutimiziaye haja zetu.

2. Tunapaswa kumwomba Mungu ambaye ndiye muweza wa yote. Sala / Maombi yetu yote yanamwelekea Mungu.  Yeye anaweza kutujibu kwa namna mbalimbali: mf. kupitia watu, viumbe wa kiroho, na hata kupitia mazingira;  hivyo sisi hatutazami ni kwa njia gani tumepokea bali tunatazama ni wapi kimetoka. Kwa hiyo tunamwomba Yeye (Mungu) aliye chanzo cha baraka zetu.

3. Tunamwomba Mungu kwa sababu Yeye ndiye muweza wa yote; vitu vyote vimetoka Kwake na hata sisi ni Wake. Katika Zaburi 33 Biblia inasema,

“…Nchi imejaa fadhili za BWANA. Kwa neno la BWANA mbingu zilifanyika, Na jeshi Lake lote kwa pumzi ya kinywa Chake. – Zab 33:5-6

Hivyo, ni Mungu ndiye aliye chanzo cha baraka zote; sala / maombi yetu yote tunayaelekeza kwake Yeye pekee.

Sasa basi; katika Injili ya Luka11:1 tumeona mwanafunzi wa Yesu akimwomba awafundishe kusali; hebu tazama jinsi Yesu anavyowaambia: “…ninyi salini hivi…” (Mt 6:9), “…Msalipo semeni…” (Lk 11:2), “…Baba yetu uliye mbinguni…” (Mt 6:9; Lk 11:2). Yesu anawaambia sala zao wazielekeze / wazipeleke kwa “…Baba yetu…” (Mungu) aliye mbinguni, na wala si mwingine. Na vile vile Yesu anazidi kutufafanulia kwamba:

“Nanyi mkiomba lo lote kwa jina Langu, hilo nitalifanya, ili Baba atukuzwe ndani ya Mwana.” - Yn 14:13

Tunapaswa kumwomba Mungu kupitia Yesu Kristo (kwa jina la Yesu). Hapo anayetenda ni Yesu ndio maana amesema: “…hilo nitalifanya…” lakini anayetukuzwa ni Mungu Baba. Hapo zingatia point hii: Hatumwombi Yesu ila tunamwomba Mungu Baba kwa jina la Yesu (yaani kupitia Yesu kunapokea kutoka kwa Mungu Baba).
Ndio maana katika Wakolosai 3:17 Biblia inasema:

“Na kila mfanyalo, kwa neno au kwa tendo, fanyeni yote katika jina la Bwana Yesu, mkimshukuru Mungu Baba kwa Yeye.” - Kol 3:17

Kwa jina la Yesu vipofu wanaona, viwete wanatembea, wafu wanafufuliwa, viziwi wanasikia, na wokovu tumeupata: Lakini shukrani zetu tunazipeleka kwa Mungu Baba kwa majibu ya sala zetu anayotupatia kupitia Yesu Kristo. Nadhani hadi hapo imeeleweka vema.
Hebu sasa tujifunze; ni kwa nini maombi yako yanaweza yasijibiwe?

Kuna mambo matatu yanayofanya maombi yako yasijibiwe:

1. Dhambi (maisha ya dhambi).
2. Kuomba vibaya.
3. Kutokuwa na imani.

1. DHAMBI (MAISHA YA DHAMBI).
Dhambi ndiyo inawatafuna wengi sana kuliko hivyo vingine viwili nilivyovitaja hapo juu. Biblia inasema kwamba:

“Kila atendaye dhambi, afanya uasi; kwa kuwa dhambi ni uasi.” – 1 Yn 3:4

Tukisoma 2 Kor 6:14 Biblia inasema hakuna urafiki kati ya haki na uasi. Ikiwa kama Mungu anatuambia sisi tusifungamane na waovu kwa namna isiyo sawa sawa; je, si zaidi ya hivyo kwa Mungu? Huwezi kupokea majibu ya maombi yako bila kufanya toba. Kabla ya kuingia kwenye maombi ni lazima kwanza wewe ujitakase (fanya toba ya kweli); na ili Mungu akusamehe nawe pia unapaswa kuwasamehe waliokukosea. Biblia inasema,

Basi, kwa kuwa mmekuwa wateule wa Mungu, watakatifu wapendwao, jivikeni moyo wa rehema, utu wema, unyenyekevu, upole, uvumilivu, mkichukuliana, na kusameheana, mtu akiwa na sababu ya kumlaumu mwenzake; kama Bwana alivyowasamehe ninyi, vivyo na ninyi.” – Kol 3:12-13

tena iweni wafadhili ninyi kwa ninyi, wenye huruma, mkasameheane kama na Mungu katika Kristo alivyowasamehe ninyi.” – Efe 4:32

“Jilindeni; kama ndugu yako akikosa, mwonye; akitubu msamehe. Na kama akikukosa mara saba katika siku moja, na kurudi kwako mara saba, akisema, Nimetubu, msamehe.” – Lk 17:3,4

“Kwa sababu hiyo nawaambia, Yo yote myaombayo mkisali, aminini ya kwamba mnayapokea, nayo yatakuwa yenu. Nanyi, kila msimamapo na kusali, sameheni, mkiwa na neno juu ya mtu; ili na Baba yenu aliye mbinguni awasamehe na ninyi makosa yenu. Lakini kama ninyi hamsamehe, wala Baba yenu aliye mbinguni hatawasamehe ninyi makosa yenu.” – Mk 11:24-26

Kuna umuhimu mkubwa sana kusamehe na kufanya toba ndipo uingie katika maombi; Ndio maana katika Waebrania 12:14, Biblia inasema:

“Tafuteni kwa bidii kuwa na amani na watu wote, na huo utakatifu, ambao hapana mtu atakayemwona Bwana asipokuwa nao.” – Ebr 12:14

Utakatifu unatangulia ndipo utapokea haja ya moyo wako. Hata uwe na imani kubwa namna gani, usipojitakasa hayo maombi yako ni sawa na kuupaka rangi upepo. Fanya toba; jinyeyekeze mbele za Mungu kwa toba ya kweli. Usijihesabie haki maana inawezekana umemkosea Mungu bila kujua. Kutenda dhambi sio lazima kuzini tu! Sin means to miss the mark! (kutofanya kwa kiwango ulichopaswa kutenda), na huo ndio uasi kwa maana haujatenda kama jinsi unavyopaswa kutenda.

2. KUOMBA VIBAYA.
Hapa kuna shida kubwa sana; watu hawa naona wapo katika makundi mawili:

i. Wanaoomba kwa tamaa zao na anasa (sio kwa utukufu wa Mungu). Biblia inasema kwamba:

Hata mwaomba, wala hampati kwa sababu mwaomba vibaya, ili mvitumie kwa tamaa zenu.”  - Yakobo 4:3

ii. Wasiojua nani wamwombe (wanaomba ovyo ovyo tu).
Hapo awali tumejifunza Yesu anasema tumuombe "Baba" katika jina Lake Yesu, hilo atafanya (Yohana 14:13); kwa maana nyepesi ni kwamba usipomwomba Mungu Baba kwa jina la Yesu hilo halifanyi, unakuwa unapoteza muda tu, na hata ukijibiwa unapokea kutoka kwa Shetani. Kuna watu wamefundishwa vibaya; utona wapo watu wanamwomba Mungu kupitia Maria, Yosefu n.k. hayo mapokeo yakijinga inabidi watu wajiepushe nayo. Tunapaswa kumwomba Mungu Baba kwa jina la Yesu, sio namna nyingine yoyote ile.

3. KUTOKUWA NA IMANI.
Unapoomba amini tayari umepokea hata kama unaona katika ulimwengu wa mwili hali bado haijabadilika. Biblia inasema,

“…imani ni kuwa na hakika ya mambo yatarajiwayo, ni bayana ya mambo yasiyoonekana.” – Ebr 11:1

Kuamini hakusubiri matokeo mwilini; bali katika roho tayari umepokea alafu matokeo ya mwilini yatafuata. Bwana Yesu anasema,

“…Yo yote myaombayo mkisali, aminini ya kwamba mnayapokea, nayo yatakuwa yenu.” – Mk 11:24

Napenda kuhitimisha somo hili kwa mfano ufuatao, Biblia inasema kwamba:

“Hata asubuhi yake walipotoka Bethania aliona njaa. Akaona kwa mbali mtini wenye majani, akaenda ili labda aone kitu juu yake; na alipoufikilia hakuona kitu ila majani; maana si wakati wa tini. Akajibu, akauambia, Tangu leo hata milele mtu asile matunda kwako. Wanafunzi wake wakasikia…
Na asubuhi walipokuwa wakipita, waliuona ule mtini umenyauka toka shinani. Petro akakumbuka habari yake, akamwambia, Rabi, tazama, mtini ulioulaani umenyauka. Yesu akajibu, akamwambia, Mwaminini Mungu. Amin, nawaambia, Ye yote atakayeuambia mlima huu, Ng'oka ukatupwe baharini, wala asione shaka moyoni mwake, ila aamini kwamba hayo asemayo yametukia, yatakuwa yake. Kwa sababu hiyo nawaambia, Yo yote myaombayo mkisali, aminini ya kwamba mnayapokea, nayo yatakuwa yenu.”  - Mk 11:12-14,20-24

Kuna mambo ya muhimu sana kujifunza katika habari hiyo: 1. Yesu aliona njaa. 2. Wakati huo haukuwa msimu wa tini lakini Yesu alitaka apate tini kutoka kwenye huo mtini. Mambo hayo mawili ni mfano halisia wa maisha yetu: Wapo watu wenye njaa (shida / uhitaji), na katika maisha yao wapo katika wakati ambao dunia dunia nzima inasema hali ni ngumu, uchumi ni mgumu, ugonjwa huo hauna tiba; wanajaribu namna mbalimbali ya kujinasua lakini hawaoni matokeo. Hali hiyo ni sawa na jinsi Yesu alivyokuwa na njaa lakini alitaka ale tini wakati ambao sio msimu wa matunda hayo. Sijui kama hapo umenielewa vema.
Yesu aliulaani mtini kisha akaondoka zake, siku ya pili yake waliporudi walikuta ule mtini umekauka. Kuna jambo la kujifunza hapa: mti ule ulikauka pale punde tu alipotamka japokuwa kwa macho ya nyama ulionesha bado haujakauka! Matokeo huanzia katika ulimwengu wa roho alafu ndipo jibu linadhihirika katika ulimwengu wa mwili. Hivyo ndivyo tunapaswa kuwa na imani. Mtu wa haki ukitamka tu tayari papo hapo imetimia, usipoteze muda kusubiri matokeo katika ulimwengu wa mwili.

Bila shaka somo hili limefanyika baraka kwako. Nakutakia baraka tele, Mungu Mwenyezi akubariki katika jina la Yesu Kristo. Amen.
Somo hili limeandaliwa nami Masanja Sabbi (+255756147354). Mungu akubariki sana.

0 MAONI:

Post a Comment

TUMA KWA RAFIKI :

Twitter FacebookMore

 
Kuhusu Huduma Hii | Masharti Ya Utumiaji Wa Tovuti Hii | Wasiliana Nasi | Tangaza Kupitia Tovuti Hii