Sunday, December 28, 2014

KUTII NENO LA MUNGU NA UTAKATIFU KWANZA.

KAMPENI YA UZIMA WA MILELE: 

"KUTII NENO LA MUNGU NA UTAKATIFU KWANZA."

Ukristo sio dhehebu; bali Ukristo ni mahusiano bora na Mungu.

Watu wengi hudhani Ukristo ni dhehebu ambalo limeanzishwa ili kuleta ustaarabu fulani katika jamii. Wakristo wengi wanaishi maisha ya kuigiza kisa tu ni wafuasi wa kanisa fulani! Wengine wanayaacha maagizo ya Mungu na kuyaheshimu mapokeo potofu ya dhehebu fulani eti kisa tu na wao wanajiita wakristo! Wengi wanaishi maisha ya maigizo, wanatenda dhambi kwa siri huku wakijiita "wapendwa"! Ndugu yangu na rafiki yangu; hapo unajidanganya wewe mwenyewe. Hakuna dhambi unayoweza kumficha Mungu. Leo ninasema na roho yako! Yachunguze matendo yako, chunguza siri za nafsini mwako; umemtenda Mungu dhambi. Umekuwa mnafiki, umekuwa na majungu japo unajiita mkristo, umekuwa mwizi japo unaitwa mpendwa, umekuwa mwongo umezaa hata nje ya ndoa yako kwa siri ukidhani Mungu hakuoni, umekuwa mshirikina na umejaa hila nafsini mwako. Unatenda ukidhani hakuna akuonaye; kumbe hapo wajidanganya wewe mwenyewe.
Biblia Takatifu inatuambia kwamba:

"Pumzi ya mwanadamu ni taa ya BWANA; Hupeleleza yote yaliyomo ndani yake." ~ Mithali 20:27.

Hakuna jambo uwezalo kumficha Mungu. Yeye anayajua mawazo yako hata kabla hujatenda jambo. Mungu anajua kuwa leo umekusudia kufanya uzinzi japo kuwa unamficha mchungaji wako! Anajua kuwa leo umetoka kufanya uzinzi japo kuwa unasema "Bwana Yesu asifiwe"!
Ichunguze nafsi yako, tubu sasa kwa maana neema bado ingalipo kwako. Wokovu sio wa maigizo, bali wokovu ni maisha halisi. Najua umeanguka mara nyingi dhambini lakini leo unayo nafasi ya kurekebisha maisha yako; Tubu sasa, la sivyo jehanam ipo kwa ajili yako na inakungoja.

Narudia tena kwa msisitizo: Ukristo sio dhehebu; bali Ukristo ni mahusiano bora na Mungu. Ukristo unaonekana katika kunena kwako, kuvaa kwako, upendo wako kwa Mungu na kwa majirani zako. Huwezi kusema Mungu hatazami uvaaji bali anatazama tu roho yako! Hapo hakika haupo salama; hicho ni kiburi tu cha uzima kinachokusumbua. Biblia inasema kuwa sisi ni barua isomwayo na watu wote (2 Kor 3:2), je ni tabia ipi uioneshayo kwa watu wasiomjua Mungu? Huko ni kuutukana wokovu wako, na hakika utatoa hesabu ya matendo yako yote. Haijarishi kuwa wewe unajiita au unaitwa mtume au nabii, haijarishi wewe ni mwinjilisti au mchungaji, haijarishi kwamba wewe ni mwimbaji au ni mwalimu, na hata kama wewe ni muumini wa kawaida tu; lakini nakuambia usipotubu leo, hakika kesho yako itakuwa ni ya majuto; itakuwa ni kilio na kusaga meno milele yote.
Biblia inapotuambia tujitenge na uovu wa kila namna (Zaburi 107:42); ni kwa sababu dhambi iingiapo unaweza ukaiona kama ni kitu kidogo tu, lakini usipoitubu na kuikemea utajikuta umejenga mazoea ya kuiona ni kitu cha kawaida tu; na hapo ndipo uovu unaumbika ndani yako. Hata kama ukikemewa utakuwa na kiburi kwa maana hiyo roho ya kuizoelea dhambi inakuandama. Dhambi sio kitu cha kuzoelea hata kidogo, dhambi imekusudia kukutenga tena na Mungu; uwe makini sana mpendwa. Leo ninaongea nawe kwa upole, ninaonge na roho yako. Rekebisha matendo yako kwa maana neema bado ingalipo kwako.
Biblia Takatifu inasema:

"Wanyofu wa moyo wataona na kufurahi, Na uovu wa kila namna utajifumba kinywa.
Aliye na hekima na ayaangalie hayo; Na wazitafakari fadhili za Bwana.
" ~ Zaburi 107:42-43

Mtu MNYOFU ndiye atakayeufurahia uzima wa milele; lakini mwovu atakataliwa mbali kabisa na Mungu. Kila jambo linayo kanuni yake, hata uzima wa milele pia unayo kanuni yake. Biblia Takatifu inatuambia kwamba:

"Tafuteni kwa bidii kuwa na amani na watu wote, na huo utakatifu, ambao hapana mtu atakayemwona Bwana asipokuwa nao;
mkiangalia sana mtu asiipungukie neema ya Mungu; shina la uchungu lisije likachipuka na kuwasumbua, na watu wengi wakatiwa unajisi kwa hilo.
" ~ Waebrania 12:14-15

Tafuta kwa bidii amani kwa watu wote pamoja na huo UTAKATIFU. Tunapoelekea katika mwaka 2015, hebu kampeni yetu iwe ni "KUTII NENO LA MUNGU NA UTAKATIFU KWANZA" Tuyakemee na kujiepusha na mafundisho potofu.Tuzingatie hili:

"KUTII NENO LA MUNGU NA UTAKATIFU KWANZA"

Ukristo sio dhehebu; bali Ukristo ni mahusiano bora na Mungu. Nawatakia nyote baraka tele katika jina la Yesu Kristo, amen.

Thursday, December 25, 2014

UKWELI KUHUSU CHIMBUKO LA SIKU KUU YA CHRISTMAS.!

UKWELI KUHUSU CHIMBUKO LA SIKU KUU YA CHRISTMAS.!


Tusiwe wanafiki, tusiwe waongo! UONGO NI DHAMBI.

Mafundisho ya Yesu kazaliwa tarehe 25 Disemba yametoka wapi? Christmas sio sikukuu ya kusheherekea tarehe ambayo Yesu amezaliwa.
Tukitazama ushahidi wa Kibiblia hauoneshi Yesu alizaliwa mwezi gani wala tarehe gani; hata pia tukitazama ushahidi wa Kihistoria nao unatubainishia kuwa Yesu Kristo alizaliwa KATIKATI YA MWAKA 6 kwenda wa 5 b.C. Hivyo basi Yesu Kristo alizaliwa miezi ya KATIKATI YA MWAKA wala sio mwishoni mwa mwaka! Mambo haya ni muhimu sana kwako Mkristo uelewe, sio unakwenda tu kama kipofu.

Kwa ushuhuda wa kweli, katika Injili zote ndani ya Biblia Takatifu hakuna mahali po pote palipoandikwa kuwa Yesu Kristo alizaliwa majira yapi wala tarehe ipi; bali tunaona tu ushuhuda wa Yesu Kristo ambaye ni Mungu aliuvaa mwili kisha akazaliwa mfano wa mwanadamu! Kuzaliwa kwa Yesu Kristo kunaelezwa wazi wazi katika Injili ya Mathayo 2:1-16, na katika Injili ya Luka 2:1-7. Tangu kuzaliwa kwa Yesu, hata wakati wa utoto wa Yesu, hata wakati wa huduma ya Yesu hapa duniani, hata wakati wa mitume, hadi kufika mwaka wa 349 AD hapakuwa na sherehe ya kuzaliwa kwa Yesu mnamo tarehe 25 mwezi Disemba kila mwaka!

JE, DESTURI HII IMETOKEA WAPI?

Mara nyingi tunapoelekea mwishoni mwa kila mwaka, tangu mnamo mwaka 350 AD, watu wengi duniani husherehekea siku kuu maarufu sana ijulikanayo kwa jina Christmas. Siku kuu hiyo huadhimishwa kila tarehe 25 ya mwezi Disemba kila mwaka, na wengi huamini kuwa ndiyo tarehe ambayo Yesu Kristo alizaliwa! Je, ni kweli kuwa Yesu alizaliwa katika tarehe hiyo (tarehe 25 Disemba)?
Kusema ukweli, kabla ya mwaka 350 AD, sherehe ya Christmas haikuwepo kabisa, na wala hapakuwepo na maadhimisho ya Yesu kuzaliwa katika tarehe 25 Disemba hadi ulipofika mnamo mwaka 350 AD wakati ambao papa wa kanisa la RC aitwae jina lake Julius I alipotangaza rasmi kuwa tarehe 25 Disemba ndiyo itakuwa siku ya kusheherekea kuzaliwa kwa Yesu Kristo! Julius I alifanya hivyo kwa lengo la kuifuta na kuifidia siku ambayo wapagani walikuwa wakisherehekea kuzaliwa kwa “mungu” wao JUA na mwanzo wa majira ya “Spring” (kuchipuka kwa mimea).

Katika majira hayo ayo pia kulikuwa na sikukuu ya wapagani wa Kirumi inajulikana sana kwa jina la “Roman Saturnalia” ambayo pia Warumi walikuwa wanampa heshima “mungu” wao “Saturn” (sayari ya Satan), ambaye wao walikuwa wanamwabudu kuwa ndiye “mungu” wao wa mavuno! Warumi walikuwa wanaadhimisha sherehe hiyo kila mnamo tarehe 19 ya mwezi Disemba na ilikuwa inaadhimishwa kwa siku saba mfululizo hadi tarehe 25 ya mwezi huo wa Disemba ndipo maadhimisho ya siku kuu hiyo yalipositishwa.

Vivyo hivyo, katika Ulaya kaskazini, pia nao walikuwa wanaadhimisha sherehe ijulikanayo kwa jina la “Yule” ambayo pia waliifanya kwa heshima ya “mungu” wao kwa kuwa katika majira hayo ndipo wakati ambao majira ya baridi yalikuwa wanamalizika na jua lilianza kuchomoza.

Kimsingi na kiukweli maadhimisho ya siku ya Christmas HAYAMO ki Biblia, kwa sababu hayo ni mapokeo tu yaliyowekwa na wanadamu, na tena SIO TAHERE SAHIHI ambayo Yesu Kristo alizaliwa. Ndio maana yapo mataifa yanayoadhimisha kuzaliwa kwa Yesu mnamo mwezi Januari, na mengine wanaadhimisha miezi mingine kulingana na mtazamo wao; Bali hayo maadhimisho katika tarehe 25 Disemba yametokana na fundisho la Julius I wa kanisa la RC ambaye aliliweka kulingana na mitazamo yake yeye mwenyewe; japokuwa neno “Christmas” tukilinyambua tunapata jina “Christ - Mas” ambalo maana yake inakuwa “Christ” maana yake ni “Kristo”, na “Mas” huenda likawa na maana ya “Misa” japokuwa neno “Misa” lenyewe linakuwa linaandikwa “Mass” yenye double “ss” sio single “s”!

Huo ndio ukweli kuhusu chimbuko la sherehe ya Christmas katika tarehe 25 Disemba. Kwangu mimi binafsi Christmass ipo kila siku wala sio tu tarehe 25 Disemba kwa maana kila siku kwangu ni Ibada ya Kristo, pia ninajua kwamba Yesu HAKUZALIWA MWISHONI MWA MWAKA, bali Yesu Kristo ALIZALIWA KATIKATI YA MWAKA WA 6 kwenda MWAKA WA 5 b.C.

 Uthibitisho huo wa Yesu Kristo kuzaliwa mnamo KATI KATI ya mwaka wa 6 kwenda wa 5 b.C (k.K) pia unatibitishwa na Biblia ijulikanayo kwa jina la Life Application Study Bible, katika ule ukurasa wa "A20" kama jinsi picha hii inavyoonesha katika sehemu hiyo iliyozungushishwa duara jekundu.
Na kwa takwimu hizo, hata mwaka wa kwanza A.D (b.K) Yesu Kristo tayari alikuwa na umri wa miak mitatu unusu! Na hapo pia panapingana na ile dhana inayosemwa kuwa Yesu alipozaliwa ndipo miaka ikaanza kuhesabiwa kwa mfumo wa A.D.
Hilo fundisho la Yesu kuzaliwa tarehe 25 mwezi Disemba ni uongo tupu na ni lazima tulipinge kabisa, tena Kanisa la Kristo tunatakiwa kulipinga na kulipiga vita vikali kabisa.

Tuutafuteni wokovu sio kuitafuta tarehe ambayo Yesu alizaliwa; Kila siku tunapaswa kukumbuka kuzaliwa kwa Yesu na thamani ya wokovu huu; sio tu katika tarehe 25 Disemba, bali kila siku tuwe katika uwepo wa Kristo. Mimi binafsi, kila siku kwangu ni Christ mass, hata leo pia. Tarehe haiokoi, bali Yesu ndiye anaokoa.


Je, wewe unasherekeaje Christmass?

Tuesday, October 21, 2014

UMEPEWA TUMAINI MAHALI PASIPO NA TUMAINI ! ! ! ~ Fahamu ukweli huhusu Purgatory (toharani)

UMEPEWA TUMAINI MAHALI PASIPO NA TUMAINI ! ! !

SHETANI AMEKUPIGA NGWALA, NAWE UMEANGUKA CHINI PUU!!! POLE KWA MAANA HUJITAMBUI, FUMBUA AKILI SASA KABLA HUJALALA FOFOFO.

Biblia inatuambia kwamba; Shetani ni "mdanganyifu", tena kazi yake ni sawa na "mwizi" ambaye ni mwaribifu, tena Shetani ni "mjanja sana"; Tazama sasa amekupa tumaini mahali pasipo na tumaini!

Purgatory (toharani)

Kwa imani ya baadhi ya makanisa yanawaambia watu kwamba ipo sehemu ya kutakasa DHAMBI NDOGO baada ya wao kufa katika hizo waziitazo DHAMBI NDOGO.
Wao wanasema hivi:

Purgatory (toharani) ni nyumba iliyopo katikati ya Mbinguni na kuzimu. Ni mahali pa kutakasia ambapo roho itaona maumivu kwa muda kidogo kabla ya kufaa kupata kibali cha kuingia mbinguni. Kwa hiyo; wao wanasisitiza: Watu waliobaki hai duniani watakapofanya maombi, kuwasha mshumaa na kutoa fedha kwenye kanisa huweza kupunguza muda ambao roho inaweza kupata machungu ya mateso ya kutakaswa katika 'Purgatory’ (Toharani).

Je! Biblia inazungumziaje fundisho hilo?

~ Biblia INAPINGA mafundisho hayo POTOFU. Tena HAKUNA DHAMBI KUWA WALA DHAMBI NDOGO "Atendaye dhambi ni wa Ibilisi..." - 1 Yoh 3:8. Tena hukumu yao ni kutupwa katika ziwa la moto wa mateo ya milele (UFUNUO 21:8)

Ukweli ni huu:

"Na kama vile watu wanavyowekewa kufa mara moja, na baada ya kufa hukumu" ~ WAEBRANIA 9:27
SASA HIVI ndio muda pekee ambao Mungu amekupatia kutengeneza mazingira mazuri ya roho yako baada ya kufa. Lakini, pindi tu utakapo kata roho, hapo ndipo MWISHO wa hesabu ya matendo yako. Kinachokuwa kimebaki kwa wakati huo ni WEWE KUISUBIRI HUKUMU ambayo itakuwa sawa sawa na jinsi MATENDO yako yalivyo. KIFO KINAFATIWA NA HUKUMU. Wafu wote wamehifadhiwa kwa ajili ya HUKUMU ambayo kila mtu atahukumiwa SAWASAWA na MATENDO YAKE MWENYEWE (soma kitabu cha Ufunuo 20:13).

Usiufanye moyo wako mgumu katika dhambi; usisubiri KUOMBEWA baada ya kufa kwako! Fanya maamuzi sahihi wakati huu ambapo neema bado ingalipo kwako. Biblia Takatifu inatuambia:

"...tazama,wakati uliokubalika ndiyo sasa; tazama siku ya wokovu ni sasa." ~ 2 Kor 6:2.

Usiiache neema hii ikupite bure! Bwana Yesu anasema:

"Hakuna mtu awezaye kuja Kwangu, asipovutwa na Baba aliyenipeleka; nami nitamfufua siku ya mwisho." ~ YOHANA 6:44.

UJUMBE HUU UNAKUHUSU WEWE ULIYEGUSWA NA INJILI HII: HACHA KUPEWA TUMAINI MAHALI PASIPO NA TUMAINI ! ! !

HAKUNA NEEMA BAADA YA KIFO. SASA HIVI NDIO WAKATI WA KUTENGENEZA MAZINGIRA YA ROHO YAKO BAADA YA KUFA; NA HUU NDIO WAKATI MUAFAKA WA KUMPOKEA YESU ILI AKUPATIE WOKOVU.

"Kwa hiyo, Tokeni kati yao, Mkatengwe nao, asema Bwana..." ~ Kor 6:17

TUMA KWA RAFIKI :

Twitter FacebookMore

 
Kuhusu Huduma Hii | Masharti Ya Utumiaji Wa Tovuti Hii | Wasiliana Nasi | Tangaza Kupitia Tovuti Hii